Header Ads Widget

NHC YATAKIWA KUWEKEZA KATIKA MJI WA KAHAMA

Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) limetakiwa kufanya uwekezaji wa majengo ya biashara pamoja na nyumba za kupangisha katika mji wa Kahama mkoani Shinyanga kutokana na mji huo kuendelea kukua kwa kasi. mwandishi wa matukio daima Munir Shemweta anaripoti kutokea Kahama


Kauli hiyo ilitolewa tarehe 25 Novemba 2021 na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula wakati wa ziara yake ya siku mbili mkoani Shinyanga kukagua utendaji kazi wa sekta ya ardhi na miradi inayosimamiwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).

Alisema, Kahama ni mji unaokuwa kwa kasi kubwa na kama Shirika la Nyumba la Taifa halijafikiria kuwekeza katika mji huo basi lijipange kuona namna gani linaweza kutumia fursa ya kukua mji huo kwa kufanya uwekezaji na kusisitiza kuwa hata kama hakuna uhitaji wa nyumba za kuuza Shirika linaweza kujenga majengo ya biashara yanayoweza kupangishwa.

"Uwekezaji wowote mtakaoufanya hapa Kahama kama hakuna walioonesha dhamira ya dhati ya kununua basi jengeni nyumba za kupanga ili kuwa na nyumba za kutosha mji unakuwa haraka" alisema Dkt Mabula.

Kwa mujibu wa Naibu Waziri wa Ardhi, kila ambapo Shirika la Nyumba la Taifa limewekeza katika majengo ya kibiashara hakuna mahali ambapo limekosa wapangaji na kadri mji wa  Kahama unavyokuwa kwa kasi bado NHC inaweza kufaidika.

Alimuagiza Meneja wa Shirika la Nyumba la Taifa mkoa wa Shinyanga   kufanya maamuzi ya haraka kwa lile eneo lililoainishwa na Manispaa ya Kahama kwa kwa ajili ya uwekezaji na kusisitiza kuwa Kahama bado inazo fursa nyingi.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kahama ambaye ni Mkuu wa Idara ya Ardhi na Maliasili Clemence Nkusa alimuambia Naibu Waziri wa Ardhi Dkt Mabula kuwa, tayari halmashauri yake ilishatenga eneo kwa ajili ya Shirika la Nyumba la Taifa kufanya uwekezaji.

Kufuatia hatua hiyo Naibu Waziri Dkt Mabula alilitaka Shirika la Nyumba la Taifa kufanya maamuzi ya haraka na kufikia Desemba mwaka huu Wizara ya Ardhi iwe imepata taarifa ya aina ya uwekezaji utakaofanyika.

Vile vile, Dkt Mabula aliitaka NHC kufikiria namna ya kufanya uwekezaji wa nyumba katika halmashauri ya wilaya ya Ushetu kutokana na halmashauri hiyo kuwa na uhitaji wa nyumba.

" Ni vizuri pia Shirika la Nyumba kuanza kufikiria kujenga nyumba katika halmashauri ya wilaya ya Ushetu maana kule kuna uhitaji mkubwa wa nyumba zikiwemo za watumishi" alisema Naibu Waziri Mabula.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI