NA FARIDA MANGUBE, MATUKIO DAIMA APP MOROGORO
Chuo Kikuu Mzumbe kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – TAMISEMI na Wizara ya Afya kimetoa mafunzo ya uongozi kwa Waganga Wakuu wa Wilaya nchini, lengo likiwa ni kuongeza ufanisi katika usimamizi wa huduma za afya na kuhakikisha uwekezaji mkubwa wa serikali kwenye sekta hiyo unaleta tija kwa wananchi.
Akizungumza wakati wa kufunga mafunzo hayo ya siku tano kwa waganga wafawidhi wa Hoptali za Halmashauri na vituo vya afya yaliyofanyika mkoani Morogoro, Prof. Tumain Nagu Naibu katibu mkuu anaeshughulikia Afya ofisi ya waziri mkuu TAMISEMI ameipongeza Menejimenti ya Chuo Kikuu Mzumbe kwa kutambua umuhimu wa kuwajengea uwezo viongozi wa afya, akisisitiza kuwa huduma bora katika vituo vya afya zinahitaji uongozi thabiti, matumizi sahihi ya takwimu na uwajibikaji.
Amesema Serikali kupitia Wizara ya Afya imeendelea kuwekeza katika miundombinu ya afya, ikiwamo kujenga vituo vya afya zaidi ya 700 na kutoa zaidi ya shilingi trilioni 1.4 katika kuboresha huduma za afya kuanzia ngazi ya msingi.
Mafunzo hayo yamewezeshwa pia na wadau mbalimbali ikiwemo Global Fund yanalenga kuwaongezea uwezo na mbinu za kisasa za uongozi, upangaji mikakati, pamoja na usimamizi wa rasilimali.
Prof. Hanry Mollel Mratibu wa Mafunzo kutoka Chuo Kikuu Mzumbe, amesema kuwa chuo kimeamua kushirikiana na serikali ili kuimarisha sekta ya afya kwa kuandaa viongozi wenye uwezo wa kushughulikia changamoto katika utoaji huduma. “Mafunzo haya yanalenga kuongeza tija na kuhakikisha uwekezaji wa serikali unaleta matokeo yanayoonekana,” alisema.
Kwa upande wake, Prof Gabriel Komba, Kaim Naibu makam kuu – Tehama, Utafiti na ushauri wa kitaaluma chuo kikuu Mzumbe, amesema kuwa washiriki wamepata mwanga mpana kuhusu uongozi bora na matumizi ya takwimu katika kufanya maamuzi..
Kwa upande wao washiriki wa mafunzo hayo wamesema mafunzo yamewajengea uwezo wa kutatua changamoto katika vituo vya afya na kuboresha utendaji kazi. “Tumeshirikishana uzoefu na tumejifunza mbinu ambazo zitaongeza ufanisi katika kuhudumia wananchi,” Walisema.













0 Comments