AFISA Madini Mkazi wa Mkoa wa Simiyu, Mayigi Makolobela, amesema mkoa huo umeendelea kufanya vizuri katika ukusanyaji wa mapato yatokanayo na Sekta ya Madini, ambapo makusanyo ya robo ya kwanza ya mwaka wa fedha 2025/2026 yamevuka malengo kwa kufikia zaidi ya asilimia 103 ya lengo lililowekwa kwa kipindi husika.
Akizungumza mkoani Simiyu, Makolobela amesema kwa mwaka wa fedha uliopita, ofisi yake ilipewa lengo la kukusanya Shilingi bilioni 4, lakini walifanikiwa kukusanya zaidi ya Shilingi bilioni 4.5.
“Kwa mwaka huu wa fedha tumewekewa lengo la kukusanya Shilingi bilioni 4.76, na hadi kufikia robo ya kwanza tayari tumekusanya zaidi ya Shilingi bilioni 1.23, sawa na asilimia 103 ya lengo la robo mwaka,” amesema Makolobela.
Ameongeza kuwa tangu kuanza kwa Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, makusanyo ya madini kupitia wachimbaji wadogo mkoani humo yamefikia zaidi ya Shilingi bilioni 17, hatua inayodhihirisha ukuaji na uimara wa sekta hiyo katika Mkoa wa Simiyu.
Aidha, Makolobela amesema Simiyu ni miongoni mwa mikoa yenye utajiri mkubwa wa madini mbalimbali ikiwemo dhahabu, shaba, madini ya ujenzi, vito aina ya Amethyst na Nikeli yanayopatikana katika wilaya za Bariadi na Busega.
Hata hivyo, amebainisha kuwa tafiti za kina bado hazijafanyika ipasavyo katika maeneo yote ya mkoa huo, jambo linaloweza kusababisha baadhi ya maeneo yenye rasilimali kutobainika mapema.
“Kama Mkoa huu utafanyiwa utafiti wa kina, kuna uwezekano mkubwa wa kugundulika mashapo mengine, hususan madini ya metali yanayoweza kuchimbwa kwa kiwango cha kati na kikubwa, hivyo kuinufaisha Serikali na wananchi kwa ujumla,” amesema Makolobela.
Katika hatua nyingine, ameeleza kuwa Mkoa wa Simiyu una vituo vitano vya ununuzi wa madini pamoja na Soko Kuu la Madini lililopo Bariadi Mjini, ambapo shughuli kuu za biashara ya madini zinafanyika kwa ufanisi mkubwa.











0 Comments