NA MATUKIO DAIMA MEDIA
MWANACHAMA wa chama cha Mapinduzi (CCM) na wakili wa kujitegemea nchini Moses Ambwindwile amejitokeza kuchukua fomu ya ubunge jimbo la Iringa mjini .
Kada huyu wa CCM amechukua fomu leo jumapili saa 2:15 asubuhi katika ofisi za CCM wilaya ya Iringa mjini .
Ambwindwile ambae alifika ofisini hapo bila ya mpambe yeyote alikabidhiwa fomu hiyo na katibu wa CCM wilaya ya Iringa mjini Hassa Makoba .
Akizungumza baada ya kuchukua fomu hiyo Ambwindwile alisema akiwa mwanachama wa CCM mwenye sifa ameona ni wajibu wake kutia nia nafasi hiyo .
Hata hivyo alivyoulizwa nini kimemsukuma kuwania nafasi hiyo alisema kuwa ni haki yake kama mwanachama na mengi ataongea muda ukifika ila si sasa.
Wakili Ambindwile ni wakili maarufu aliyewahi kuhudumu ndani ya mhimili wa Mahakama ya Tanzania kama Msaidizi na Mshauri wa Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Kwa sasa, yeye ni Mkurugenzi na Mwanzilishi wa Kampuni ya Sheria ya The Icon Law Corporate Attorneys, iliyopo katika Jengo la Law House, Mjini Iringa.
Aidha, ni Mwenyekiti wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) – Kanda ya Iringa na Njombe.
Wakili Ambindwile ni Mshauri wa Masuala ya Kodi anayetambuliwa rasmi na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), na pia Katibu wa Umoja wa Washauri wa Kodi mkoa wa Iringa, chombo kinachowaleta pamoja wataalamu wa kodi kwa madhumuni ya kubadilishana maarifa, kutoa elimu na kushirikiana na serikali katika kuboresha mifumo ya mapato.
Kwa heshima ya mila na utamaduni wa mkoa wa Iringa, hivi sasa Ambindwile pia ni Wakili Binafsi wa Mtwa wa Wahehe, Adam Mkwawa wa Pili.
Mwaka 2023, Ambindwile akiwa mwenyekiti wa TLS aliunda na kuongoza jopo la mawakili waliomwakilisha bila malipo mjane aliyekuwa amehukumiwa kifungo cha miaka 22 na Mahakama ya Mkoa wa Iringa kwa kosa la kupatikana na vipande 12 vya nyama ya swala.
Kupitia rufaa iliyowasilishwa Mahakama Kuu ya Tanzania, adhabu hiyo ilibatilishwa na Mheshimiwa Jaji Mugeta, na mjane huyo aliachiliwa huru.
Mbali na nafasi hizo, Ambindwile ni Mjumbe wa Bodi mbalimbali, Pia ana sifa za kikuregenzi na ukatibu wa taasisi na mashirika ambaye amefuzu na kutambuliwa rasmi na Taasisi ya Wakurugenzi Tanzania (IoDT).
Huku akiwataka wagombea wote kuzingatia kanuni na makatazo ya chama .
0 Comments