MKUU wa Mkoa wa Simiyu, Kenani Kihongosi (kulia) akipokea Shuka 100 kutoka kwa Mbunge wa Viti Maalumu (CCM) Mkoa wa Simiyu, Esther Midimu ambazo zitagawiwa kwenye Hospitali za wilaya.
Na Costantine Mathias, Simiyu.
MBUNGE wa Viti Maalumu (CCM), Mkoa wa Simiyu, Esther Midimu ameadhimisha siku ya Wanawake Mkoani humo kwa kukabidhi shuka 100 za Hospitalini ambazo zitagawiwa katika vituo vya kutolea huduma za afya.
Msaada huo umekuja kwa wakati muafaka, baada ya serikali ya Dk. Samia Suluhu Hassan kuboresha Mazingira ya utoaji huduma za Afya kwa kujenga Zahanati, Vituo vya Afya, Hospitali za Halmashauri na Wilaya, Hospitali za Mkoa, Kanda na Rufaa.
Akizungumza mara baada ya kukabidhi msaada huo March 3, 2025, akiwa Busega, Midimu amesema anatoa shuka hizo ili kuunga Mkono jitihada za Serikali katika kuboresha na kuimarisha upatikanaji wa huduma za Afya.
Ameongeza kuwa, Shuka hizo zitagawiwa kwenye Hospitali tano za Mkoa wa Simiyu ambazo ni Hospitali ya wilaya ya Busega, Itilima, Meatu, Maswa na Bariadi na kwamba kila Hospitali itapata shuka 20.
"Shuka hizo zitapunguza uhaba waliokuwa nao kwenye Hospitali zetu...naunga mkono juhudi za Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ambaye amejikita kuboresha majengo ya kutolea huduma ya Afya pamoja na vifaa Tiba" amesema Midimu.
Akipokea shuka hizo, Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Kenani Kihongosi @kenan amempongeza Mbunge huyo kwa kutoa msaada wa kibinadamu ambao utasaidia wagonjwa hospitalini.
Mwisho.
0 Comments