Header Ads Widget

KAMPENI YA MAMA SAMIA YASAIDIA WANANCHI KUTATUA CHANGAMOTO ZA KISHERIA.

 

Hamida Ramadhani,

Matukio Daima App Dodoma.

WAZIRI wa Katiba na Sheria,Dk Damas Ndumbaro amesema kupitia kampeni ya Mama Samia Legal Aids Compain (MSLAC) wamebaini  wananchi  bado wanachangamoto za kisheria katika mambo manne ambayo ni ukatili wa kijinsia,migogoro ya ardhi, ndoa na ardhi. 

Kauli hiyo ameitoa leo Jumatatu,Januari 20,2025 wakati akizungumza na Waandishi kuhusiana na kampeni ya Mama Samia Legal Aids Compain (MSLAC) katika mikoa 6 ambayo inatarajiwa kuanza Januari 24 mwaka huu.

Waziri Ndumbaro amesema kupitia kampeni hiyo walifika katika mikoa 11 na changamoto zilizojitokeza kwa wingi ni  ukatili wa kijinsia,migogoro ya ardhi, ndoa na ardhi. 

Amesema kwenye sekta ya ardhi wamebaini ubabaishaji ni  mwingi ambapo amemwomba Waziri wa Ardhi,Deogratius Ndejembi kumtumia orodha ya migogoro sugu ili baada ya kampeni hiyo waanze kuishughulikia.

"Katika sera yetu ya utoaji haki tutahakikisha  wananchi wanapata haki na wanapata elimu ya kisheria,"amesema Waziri Ndumbaro.

Amesema waliopo vijijini wana kiu ya haki ndio maana Rais aliunda Tume ya Haki jinai ambayo ilibainisha umuhimu wa haki kumfikia Mwananchi.

Amesema kupitia kampeni hiyo waliweza kuwafikia watu  175,119 ambapo  asilimia 49 ni  wanawake na 51 ni wanaume ambapo walitatua jumla ya migogoro  3162 

"Hizi takwimu wanaume ni wengi kuliko wanawake ni takwimu nzuri tu,unaona Mpango huu unamsaidia Mwananchi kuzalisha zaidi na programu hii ni mkombozi kwa wanyonge hasa wale ambao hawana uwezo wa kupata mawakili,"amesema Waziri Ndumbaro

Amesema Mpango huo unamsaidia mnyonge kupunguza malalamiko katika sekta ya sheria.

Aidha amesema Januari 24 mwaka huu watazindua kampeni hiyo kwa mikoa 6 Mkoani Kigoma.

Ameitaja mikoa mingine watakayofika ni,Kilimanjaro,Geita,Katavi,Tabora na Mtwara,

"Katika mikoa hiyo tutakuwa Januari tu na  katika Kila Halmashauri wataenda Kata 10 katika Kila Kata watatumia siku 9 na huduma  zitatolewa bure kwa wananchi,"amesema 

Amesema wataanzia Januari 24 mkoani  Kigoma kisha Katavi,Tabora na Mtwara ambapo Januari  25 watakuwa Geita na Januari  29 watamalizia Kilimanjaro.

Waziri Ndumbaro amewaomba wananchi kujitokeza kwa wingi ili waweze kupata msaada wa kisheria.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI