KATIBU Tawala Mkoa wa Simiyu Prisca Joseph Kayombo, ametembelea ofisi za Umma na kuwahimiza watumishi wa Umma kujitokeza kujiandikisha kwenye Daftari la Makazi ili waweze kushiriki kwenye uchaguzi wa serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika Nov 27, 2024.
Katibu Tawala huyo ametembelea Shirika la Ugavi wa Umeme Nchini (TANESCO) pamoja na Watumishi wengine wa Taasisi mbalimbali Mkoani Simiyu ili waweze kupata haki yao ya Msingi ya kuchagua Viongozi watakaowaongoza katika Mitaa yao.
Akizungumza na watumishi wa Tanesco, katika muendelezo wa zoezi la kuhamasisha makundi mbalimbali Mkoani Simiyu, Bi. Prica amewataka kujitokeza kwa wingi kujiandikisha.
Amewataka watumishi hao kutochanganya zoezi la maboresho ya Daftari la kudumu la Wapiga kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu na Daftari la wapiga kura za viongozi wa Serikali za Mitaa.
Amewataka pia kuwa mabalozi wa kuhamasisha Wananchi kujitokeza katika vituo vya kujindikisha ili waweze kuwa na sifa ya kupiga kura kuwachagua Viongozi wa Serikali za Mitaa.
Meneja Tanesco Mkoa wa Simiyu Bi.Alistidia Clemence amemhakikishia Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu huyo kuwa, Watumishi wote wa Tanesco Mkoani humo watajiandikisha katika orodha ya wapiga kura za viongozi wa Serikali za Mitaa.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Ofisi ya Rais -TAMISEMI uchaguzi wa Serikali za Mitaa Nchini utafanyika Tarehe 27 Novemba 2024.
0 Comments