Mratibu Kitaifa wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC),Wakili Onesmo Olengurumwa amewahasa Watetezi wa haki za Watoto Nchini kutokalia kimya matukio ya ukatili wa Watoto badala yake amewataka kujitokeza kukemea na kutaka uwajibikaji wa mamlaka zenye wajibu wa ulinzi wa haki za raia.
Ameyasema hayo leo Julai 31, 2024 katika semina ya siku mbili ambayo inawakutanisha Watetezi wa haki za Watoto ambayo imeandaliwa na THRDC kwa kushirikiana na wadau wengine, ambapo amesema kuwa Watetezi wa haki za Watoto wanayo nafasi ya kubwa ya kusaidia katika jitihada za kukabiliana na matukio mbalimbali ya ukatili kwa watoto, hususani kipindi hiki ambacho kuwepo na matukio ya utekaji na vitendo vya ulawiti na ubakaji kwa watoto.
"Tunafahamu hali ya ulinzi wa Mtoto Nchi hii imekuwa na changamoto nyingi sana Ripoti ya Jeshi la Polisi juzi ilionesha utekaji umekuwa mkubwa, kwa mfano mwaka jana tu watoto zaidi ya 73 kwa mujibu wa ripoti hiyo, tumeona masuala ya ulawiti na ubakaji yote yamekuwa matatizo makubwa ambayo hawa Watetezi wa haki za binadamu wanapaswa kwenye kukemea, kufuatilia na hata kuwajibisha zile taasisi ambazo zinahusika na ulinzi wa haki za Kiraia."amesema Olengurumwa
Amesema wana jukumu la kukemea pale wanapoona kuna dalili au vitendo vya ukiukwaji wa haki za Watoto kwa sababu ni sehemu ya majukumu yao.
Aidha Mratibu Kitaifa wa Tanzania Children Rights Forum, Ombeni Kimaro, amesema kuwa uelewa mdogo uliopo katika jamii juu ya masuala yanayohusu haki za Watoto ni sababu inayopelekea vikwazo katika ulinzi wa haki za Watoto.
Amewahasa wazazi ,walezi na jamii kwa ujumla kuwa mfano bora katika kuhakikisha wanasimamia na kulinda haki za Watoto, ambapo amesema kwa upande wao wamekuwa wakichukua hatua mbalimbali kuhakikisha haki za mtoto zinalindwa, ikiwemo kushirikiana na Serikali.
Washiriki wa semina hiyo wametokea kwenye Mikoa nane ikiwemo mkaoa wa Dar es Salaam, Morogoro, Dodoma na Singida, ambapo yatahitimishwa kesho August 2024.
0 Comments