Na Fadhili Abdallah,Kigoma
WAZIRI Mkuu Kassim Majaliwa amezindua zoezi la uandikishaji wa daftari la kudumu la wapiga kura huku akiwataka watanzania wote kujitokeza kujiiandikisha na kuboresha taarifa zao katika daftari hilo.
Waziri Mkuu Majaliwa amesema hayo Akizungumza kwenye uzinduzi wa daftati la kudumu la wapiga kura uliofanyika uwanja wa Kawawa manispaa ya Kigoma Ujiji mkoani Kigoma akisema kuwa zoezi la uboreshaji wa daftari kudumu la Wapiga kura linawuhusu watanzania hivyo hawana budi kutumia fursa hiyo sasa ili kutumiza haki yao ya kikatiba.
Kutokana na hilo amewataka Watanzania wote kusimamia kwa karibu utekelezaji wa zoezi hilo wakiwemo mawakala wa vyama vya siasa kuzingatia uzalendo wa nchi yao kwa kuhakikisha watu wanaondikishwa kwenye daftari la kudumu la wapiga kura ni Watanzania ili watu ambao siyo watanzania wanaotaka kujipenyeza kuandikishwa wasipate nafasi hiyo.
Pamoja na hilo alisema kuwa uandikishwaji mwaka huu umeboreshwa kwa kiasi kikubwa ambapo zoezi hilo unaanzia kwenye simu ya mkononi ikiwemo simu za viswaswadu ambayo itawezesha kila Mtanzania kushiriki kikamilifu kwani mpango huo unatekelezwa ili kupunguza msongamano, kupunguza muda wa kukaa vituoni na kulifanya zoezi kuwa rahisi.
Aidha katika uzinduzi huo Waziri Mkuu amevitaka vyama vya siasa ambao ndiyo wadau wakubwa wa uchaguzi huo kutoa elimu kwa wanachama wao kuhusu zoezi hilo lakini pia kuweka mawakala ambao watasimamia zoezi hilo kwenye vituo akitaka mawakala hao kutolewa kwenye maeneo husika ya vituo na kuwa na uzalendo na nchi yao.
Waziri Mkuu Majaliwa pia ameyaasa mashirika yasiyo ya serikali yaliyoteuliwa kutoa elimu kwenye zoezi la uandikishaji na uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura kuzingatia majukumu yao kulingana na maombi yao na zoezi lenyewe badaya la kufanya mambo ambaayo hayasiaani na taratibu za daftari wala uchaguzi.
Katika uzinduzi wa zoezi hilo Waziri Mkuu Majaliwa alitoa agizo kwa idara ya uhamiaji mkoa Kigoma na nchi nzima kwa jumla kutembelea vituo na kufanya uhakiki wa watu wanaoandikishwa kuwa ni Watanzania na kufanya kazi taarifa watakazopata kuhusu watu wanaotaka kujiandikisha ambao siyo Watanzania
Awali akitoa taarifa kwa Waziri Mkuu, Mwenyekiti wa Tume huru ya Taifa ya uchaguzi nchini (INEC), Jaji Jacob Mwambegele alisema kuwa Katika uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura mwaka huu 2024 kutakuwa na jumla ya vituo 40,126, ambapo kati ya vituo hivyo, 39,709 ni vya Tanzania Bara na vituo 417 ni vya Zanzibar.
Jaji Mwambegele alisema kuwa hilo ni ongezeko la vituo 2,312 ikilinganishwa na vituo 37,814 vilivyotumika kuandikisha wapiga kura mwaka 2019/2020 huku kukiwa na ongezeko la wapiga kura wapya milioni 5.5,wapiga kura milioni 4.3 wataboresha taarifa zao na wapiga kura 594,494 wataondolewa kwenye Daftari kwa kukosa sifa za kuendelea kuwepo kwenye Daftari hivyo baada ya uboreshaji inatarajiwa kuwa Daftari litakuwa na jumla ya wapiga milioni 34.7.
0 Comments