Wananchi wa kijiji Cha Ikang'asi tarafa ya Lupembe wilayani Njombe wakimsikiliza mkuu wa mkoa wa Njombe Mhe.Antony Mtaka
Na Gabriel Kilamlya Matukio DaimaAPP NJOMBE
Zaidi ya kaya 300 katika kijiji cha Ikang'asi wilayani Njombe zimeridhia kuanza kwa mradi wa kilimo cha parachichi kinachotarajiwa kuwekezwa kwenye ekari elfu 60 kati ya ekari elfu 89 zilizopimwa na serikali kwa ajili ya uwekezaji huo.
Mradi huo ulibuniwa na mkuu wa mkoa wa Njombe Antony Mtaka ambaye amelazimika kufika kijijini hapo na kufanya mkutano wa hadhara na wananchi akiongozana na Kamati ya ulinzi na usalama huku akiweka wazi faida za mradi huo pamoja na kila kaya kulimiwa ekari 10 za parachichi.
Kutokana na ufafanuzi wa kina toka kwa mkuu wa mkoa wa Njombe baadhi ya wananchi wa kijiji cha Ikang'asi akiwemo Nathan Hongoli,Mathias Mpangile,Scholastica Witulo na Ignas Mwalusekemalile wamekiri kuuelewa vyema mradi huo na kubariki uwekezaji huo.
Ofisa Mtendaji wa kijiji cha Ikang'asi Christopher Hongoli na Vasco Mgunda diwani wa kata ya Mfiriga wamesema endapo mradi huo utatekelezwa kama mkuu wa mkoa alivyopanga basi wananchi watakuwa kwenye hali nzuri ya kiuchumi na maendeleo makubwa yatapatikana kijijini hapo.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Njombe Christopher Sanga amewataka wananchi wa Kijiji hicho kwenda kuchangamkia fursa mbalimbali pindi mradi huo utakapoanza.
Hat hivyo maeneo mengine ya mradi huo yatahusisha kilimo cha aina mbalimbali zikiwemo mbogamboga,Nanasi pamoja na maeneo ya viwanda,michezo,Hotel na Nyumba za watakaokwenda kuwekeza.
0 Comments