Na Editha Karlo,Kasulu
MBUNGE wa viti maalumu kundi la wanawake mkoa wa Kigoma Zainab Katimba ameutaka umoja wa wanawake( UWT )mkoani humo kuanzisha miradi mbalimbali ya kiuchumi ili kukuza maendeleo ya umoja huo.
Katimba ametoa wito huo wakati akizungumza na wajumbe wa (UWT ) wilaya ya Kasulu na kusisitiza kuwa miradi hiyo ikianzishwa itasaidia kuongeza kipato na hivyo kurahisisha utekelezaji wa shughuli mbalimbali za umoja huo.
'' Binafsi nilianza kuliona hili nikawaletea mradi wa mashine ya kusaga na kukoboa ambayo naamini ikianza kufanya kazi itasaidia kuongeza kipato cha umoja wetu lakini natamani sana tuanzishe miradi mingi ya (UWT) ili tuweze kujisimamia zaidi kifedha,,amesema Mh, Katimba
Aidha katimba ameahidi kutoa fedha ya mtaji mbegu kwa ajili ya kuanzisha mfuko wa kukopeshana kwa wanawake wa UWT wilaya ya Kasulu ili kiwe kianzio kwa wanawake kukopeshana na kuanzisha miradi midogo midogo ya kiuchumi.
'' Nafahamu wengi wetu hapa tupo kwenye vikundi mbalimbali vya vikoba ambavyo vimekuwa mkombozi kwa wanawake na mimi katika kuliendeleza hilo nitatoa kianzio cha shilingi milioni tatu natumai viongozi wetu wataweka utaratibu mzuri ili angalau tuwe tunakopeshana kidogokidogo na kuanzisha miradi,,amesema Mh, Katimba.
Aidha mbunge huyo amewataka wanawake kuendelea kudumisha umoja na mshikamano miongoni mwao akisisitiza kundi hilo kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi za uongozi katika chaguzi mbalimbali zijazo.
0 Comments