Na Fadhili Abdallah,Kigoma
MBUNGE wa jimbo la Buhigwe mkoani Kigoma Felix Kavejuru ameongoza harambee ya kanisa la FPCT Rusaba wilaya ya Buhigwe mkoani Kigoma kwa ajili ya ununuzi wa gari la Mchungaji Kiongozi wa kanisa hilo ambapo kiasi cha shilingi milioni 13.8 zimepatikana.
Katika harambee hiyo Mbunge huyo alichangia kiasi cha shilingi milioni 1.5 huku akilitaka kanisa kuhimiza waumini wa kanisa hilo kushiriki kwenye shughuli za maendeleo za kukuza uchumi.
Pamoja na hotuba hiyo kanisani pia mbunge huyo alihutubia mkutano wa hadhara kwenye kijiji cha Rusaba wilaya ya Buhigwe mpakani mwa Tanzania na Burundi ambapo amewataka wananchi wa mkoa Kigoma kutumia fursa ya kibiashara na masoko iliyopo kwenye nchi za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo ambapo alisema kuwa kwa sasa nchi ya Burundi ina amani hivyo fursa za kufanya biashara na nchi hizo ni kubwa.
Alisema kuwa pamoja na biashara nyingine za viwandani lakini biashara ya mazao ni kubwa hasa Mashariki ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo na Burundi na kutaka wananchi wa mkoa Kigoma kutumia fursa ya kuimarishwa kwa miundo mbinu mbalimbali ya mkoa mkoa kuimarisha shughuli zao za kiuchumi hasa kilimo na kutumia fursa ya kilimo biashara iliyopo kwenye nchi hizo.
Akitoa taarifa ya harambee hiyo Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la FPCT Rusaba wilaya ya Buhigwe, Mchungaji Ayubu Kihoza alisema kuwa kiasi cha shilingi Milioni 13.8 kimepatika fedha taslim ikiwa ni shilingi milioni 4.09, ahadi za watu binafsi shilingi mlioni 4.02 na ahadi za makanisa zikiwa shilingi milioni 5.7 na Mbunge Kavejuru akichangia shilingi milioni 1.5.
Upande wake Mchungaji wa FPCT Mwanga, Zakharia Andrea alisema kuwa wameona fursa ambazo zimefanywa na serikali katika suala zima la uchumi na biashara na kuimarishwa kwa miundo mbinu kunawapa nafasi ya kuhimiza waumini wao kushiriki kwenye shughuli za maendeleo za kiuchumi.
0 Comments