Na Matukio Daima Media
ASKARI mmoja wa wanyamapori amejeruhiwa usoni na mguuni wakati akipambana kumuua mmoja kati ya Simba aliyekuwa akitishia maisha ya wananchi wa wilaya ya Kilolo mkoani Iringa .
Akizungumza na Matukio Daima Media katika uwanja wa Luganga wilayani Kilolo ambako Simba aliyeuwawa alikuwa ameletwa Leo asubuhi kamishina msaidizi wa hifadhi ya mamlaka ya usimamizi wa wanyamapori Tanzania (TAWA ) Joachim Makwai alisema kuwa matukio ya Simba yalianza toka Juni 13 mwaka huu kwa Simba kushambulia mifugo ya wananchi .
Alisema kuwa kutokana na matukio hayo kuendelea kuwa tishio askari wa TAWA walianza ufuatiliaji wa karibu na kuweka mitego katika maeneo yote ambayo Simba wamepita na kuua mifugo .
Hata hivyo alisema kuwa juzi hao walikuwa wameua nguruwe katika kijiji cha Iramba wilaya ya Kilolo hivyo askari hao walifanikiwa kuweka mitego katika eneo ambalo Simba hao walikuwa wakilala .
Kuwa kazi hiyo ilifanywa na TAWA ,taasisi ya utafiti wa wanyamapori Tanzania na madaktari wa mifugo ambao walifanikisha kumnasa mmoja kati ya Simba hao kwa mitego na eneo ambalo alikuwa amenasa lilikuwa ni vigumu kumfikia Simba huyo na kumlaza kwa kumchoma Sindano ya usingizi na ndipo walipoamua kutumia bunduki kupambana nae.
" Eneo ambalo Simba huyu alikuwa amenasa ni sehemu ya ardhi oevu na ilikuwa vigumu kumfikia kumchama sindano ya kumlaza ili kumkamata akiwa hai ndipo tulipoamua kutumia risasi kwa kumpiga na kutokana na kutaka kujiokoa alimrukia askari wetu mmoja na kumjeruhi usoni japo tayari alikuwa hana nguvu kutokana na risasi alizokuwa amepigwa " alisema Makwai
Kuwa askari huyo aliyejeruhiwa anatambulika kwa jina la Charlesy Mafuru kutoka TAWA na baada ya kujeruhiwa alikimbizwa hospitali ya wilaya ya Kilolo ambako alipatiwa matibabu na kuruhusiwa .
Makwai alisema hadi sasa bado wanaendelea kufanya msako kama kuna simba mwingine zaidi baada ya Simba huyo jike kuuwawa .
Alisema simba hao waligawanyika katika makundi mawili kundi moja alikuwa eneo la jimbo la Kalenga kijiji cha Maboga ambako inasadikika alirudi hifadhini ya Taifa ya Ruaha baada ya matukio ya mifugo kuuwawa kutotokea tena ila kundi la pili ni hilo la simba mmoja alielekea wilaya ya Kilolo ambako tayari simba ameuwawa .
Hivyo aliwataka wananchi kuendelea kuwa waangalifu zaidi hasa nyakati za jioni na usiku ambao ni muda wa Simba kuwinda .
Joseph Tengelapo diwani wa kata ya Dabaga alisema kuwa kabla ya simba huyo kuuwawa alikuwa ameua mbuzi ,ng'ombe na Nguruwe katika vijiji vya kata yake ili hawakufanikiwa kuwapata simba hao .
Hata hivyo baada ya matukio hayo wananchi wake wa vijiji viwili vya kata hiyo waliamua kujifungia ndani muda wote bila kutoka nje kutokana na hofu kubwa ya kuliwa na simba hadi juzi Simba huyo alipofanya tukio la kula nguruwe eneo la Shule ya Msingi Iramba .
Alisema kufuatia tukio hilo ndipo askari hao wa wanyamapori waliamua kuweka mtego kijijini hapo na kufanikiwa kuua simba huyo Leo asubuhi .
Diwani huyo aliishuruku serikali na askari wa wanyamapori ambao wamefanikisha kuuwawa kwa simba huyo kwani hofu ya wananchi wake ilikuwa kubwa sana na hata shughuli za uzalishaji mali zilisimama kwenye kata yake kwa hofu ya simba .
Kwa upande wake askari aliyejeruhiwa na simba Joachimu Mafuru alisema kuwa asubuhi walifanmikiwa kwenda eneo ambalo walitega mtego huo akiwa na askari wenzake watano na baada ya kufika eneo la mtego walisikia mgurumu wa simba ila hawakujua yupo eneo gani .
Hivyo wakati wametawanyika kumtafuta Simba huyo ndipo askari mwenzake alifanikiwa kumpiga risasi Simba kifuani na wakati Simba akijaribu kujitetea ndipo alipokutana naye uso kwa uso akitaka kumrukia ndipo alipojiokoa kwa kumfyatulia risasi mfululizo kifuani hadi Simba huyo alipoanguka chini .
Alisema pona yake ni aina ya bunduki ya SMG aliyokuwa akiitumia ndio iliyomuokoa kutokana na kutoa risasi mfululizo zilizomlenga simba kifuani .
" Hili ni tukio langu kubwa la pili kunusurika kifo na wanyama tukio jingine ambalo sitalisahau ni lile na kupambana na nyati aliyejeruhiwa na nilifanikiwa kumuua"
Mkuu wa mkoa wa Iringa Halima Dendego mbali ya kuwashukuru askari hao kwa ujasiri walioonesha wa kufanikisha kuua simba huyo bado aliungana na wananchi kwa kuwachangia pesa kiasi cha Tsh 500,000 kama ahsante huku wananchi wakichangia shilingi 64000 kuwapongeza askari hao .
Mkuu huyo wa mkoa alisema utaratibu wa kuwapongeza zaidi askari hao unafanyika na kuwataka wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa askari hao na viongozi wa serikali ya wilaya na mkoa kutoa taarifa sahihi za Simba katika maeneo yao na kuachana na taarifa za upotoshaji .
Simba hawa Walivamia Makazi ya wananchi wa Jimbo la Kalenga na Kilolo toka Juni 13 mwaka huu na hadi Sasa ni zaidi ya siku 34 na wameuwa Ng'ombe na Nguruwe zaidi ya 56 pamoja na kuku mmoja
0 Comments