Na Matukio daima,Mbeya
SHIRIKA lisilo la kiserikali la wadau wa kilimo (ANSAF,) limeweka mikakati ya kuboresha kilimo cha zao la kahawa kwa wakulima ili kuongeza tija ya uzalishaji na kufikia malengo.
Mkurugenzi mtendaji wa Shirika hilo ,Honest Mseri amesema leo kwamba wamelazimika kufanya hivyo kutokana na uzalishaji kuwa mdogo .
Mkutano huo wa siku moja ulioshirikisha wadau , maafisa kilimo wa serikali , wafanyabiashara , sekta binafsi pamoja na wakulima kutoka mikoa mitatu ambayo ni , Mbeya, Songwe na Ruvuma .
Amesema kuwa kutokana na zao la kahawa kuwa kongwe hapa nchini ni wakati sasa wa kuboresha mifumo ya upatikanaji wa miche bora ambayo italeta tija kubwa katika uzalishaji na mikoa husika kufanya vizuri zaidi kwenye kilimo hicho.
“ Siku zote wakulima wamekuwa wakiangalia zao ambalo linawapatia kipato hivyo ili kuweza kuwavutia ni lazima kuwa na mbegu bora ambayo itakuwa msaada kwa mkulima .”amesema.
Amesema kuwa wastani wa asilimia 90 ya kahawa inasafirishwa kwenda nje ya nchi na ndio sababu kubwa ya kuwakutanisha wadau ili kutengeneza soko la ndani na kuvutia wanunuzi wengi ili kuboresha kipato cha wakulima.
Amesema kuwa lengo kubwa ni kuona zao la kahawa lina fursa kubwa ya kuendelea kutoa fursa za ajira hususan maeneo mengi yanayolima yanakuwa na Maendeleo makubwa ukilinganisha na maeneo yasiyolima kahawa ili kuongeza kushawishi kuzalisha kwa tija kubwa..
Kwa upande wake ,Labeli Ulomi ni Meneja uzalishaji kampuni ya ukoboaji Kahawa Mbimba iliyopo mkoani Ruvuma amesema kuwa Mkoa wa Ruvuma una ardhi kubwa ambayo inafaa kwa kilimo ambayo bado haijatumika na yenye rutuba na halmashauri ya Mbinga pekee ina kiasi cha hekta 25,000 ambazo zingeweza kulima kahawa lakini hazijaweza kutumika kwa ajili ya kilimo cha kahawa hivyo ni ni fursa kubwa kwa kilimo cha kahawa ikifuatiwa na Nyasa ambayo ina hekta zinazozidi 6,000 ambazo hazijatumika kwa ajili ya kilimo cha kahawa .
Dismas Pangalasi ni Meneja wa programu za utafiti wa zao la Kahawa Kanda ya Mbeya ,amesema kuwa jukumu lao ni kutoa mafunzo kwa wakulima pamoja na kuzalisha miche bora ya kahawa na kwamba kwa mwaka 2022/2023 wameweza kuwafikia wakulima 7,640 katika mkoa wa Mbeya na Songwe kwa wilaya nne na kutoa mafunzo ya ,mabadiliko ya tabia nchi kwa wakulima 9,530 .
Alitaja fursa kubwa wanaweza kuzipata wakulima ni kutoka Taasisi ya utafiti wa kahawa ambayo ipo kwenye maeneo yao ,pia wana aina 13 bora za kahawa ambazo zinazalishwa kituo cha utafiti Tacri Mbimba na kuwa aina hizo za mbegu hazishambuliwi na wadudu.
Akizungumza na majira mmoja wa wakulima wa kilimo cha Kahawa , Jeremiah Mwaje amesema kuwa kwa muda mrefu amekuwa akijishughulisha na kilimo cha Kahawa ambacho mwanzo alikuwa akipata kahawa kwa wingi lakini hivi sasa changamoto ipo kwenye soko na ubora wa mbegu.
0 Comments