ASKOFU wa kanisa la ACTS Felloshp Tanzania DKt Mpeli Mwaisumbe amesema kazi inayofanywa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan katika Taifa ni kubwa na utendaji wake unajidhihilisha kuwa ni Rais bora Mwanamke Afrika hivyo jukumu la watanzania kuendelea kumuombea ili azidi kuliongoza Taifa vema huku akimuomba kutowaonea haya vigogo wote waliotajwa kwenye ripoti ya mdhibiti na mkaguzi wa hesabu za serikali (CAG).
Akitoa salam za Pasaka leo mara baada ya ibada katika kanisa la ACTS Felloship Centre Iringa mjini Dkt Mwaisumnbe alisema kuwa mbali ya Taifa kuendelea kujivunia mafanikio makubwa ambayo yameletwa na serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Dkt Samia ,ila bado kuna mambo ambayo yanakwenda ndivyo sivyo na kila mmoja anawajibu wa kukemea kwa nguvu zote .
Kuwa hivi karibuni imetoka ripoti ya CAG na katika ripoti hiyo kuna watu wametajwa kuhusika na matumizi mabaya ya fedfha za umma fedha ambazo kama zingetumika vizuri zingesaidia kuleta maendeleo kwenye Taifa hivyo bila kuangalia sura ya kiongozi ni vizuri fedha hizo zikarejeshwa ili zielekezwe kwenye miradi ya maendeleo .
" Mheshimiwa Rais wetu mama Dkt Samia Suluhu Hassan amekuwa mfano mwema wa uongozi kwenye Taifa na hata bara zima la Afrika hivyo tunahitaji kumuunga mkono wote kwa nguvu zetu zote sisi viongozi wa dini tuendelee kumuombea afya njema ila na wale waliopo serikalini wanaomsaidia wawe waadilifu wa fedha za umma" alisema askofu Dkt Mpeli .
Akizungumzia kuhusu maadili katika jamii askofu Dkt Mpeli alisema ni wajibu wa jamii kuendelea kukemea vitendo vya ushoga na usagaji vinavyoendelea kuchipua katika jamii kwani vitendo hivyo ni chukizo mbele za Mungu na kila mzazi ama mlezi anawajibu wa kutoa elimu kwa watoto wake ili kuepukana na vitendo viovu vya ndoa za jinsia moja .
Alisema Yesu Kristo alibeba dhambi zetu na hata kufa msalabani kwa ajili ya wote wenye dhambi hivyo wakati wakristo kote ulimwenguni wanaposherekea sikukuu ya kufufuka kwake Yesu Kristo ni vema kuachana na mambo yote maovu yasiyompendeza Mungu ili Yesu kristo afufuke ndani ya mioyo na sio katika mavazi ama chakula .
0 Comments