Mwandishi wetu_Musoma
Taasisi ya Tanzania Media for Maritime and Fisheries Development (TMFD) imeiomba Serikali kupitia wizara ya mifugo na uvuvi kuwasaidia wavuvi wa Mwalo wa Busekera, Halmashauri ya Musoma Mkoa wa Mara ambao wamepoteza zana za o za uvuvi kufuatia mvua kubwa iliyonyesha usiku wa kuamkia Machi 21, 2023 iliyoambatana na wimbi kubwa katika Ziwa victoria lililosababisha hasara kwenye zana za uvuvi.
Mkurugenzi wa TMFD Bwana Edwin Soko amesema katika mvua hizo zaidi ya mitumbwi 70 ilipasuka kutokana na kurushwa na mawimbi toka majini hadi nchi kavu baada ya nanga za mitumbwi hiyo kuzidiwa nguvu na kusababisha mitumbwi hiyo kugongana na kupasuka pamoja na makokoro kufikiwa kwenye mchanga.
TMFD imefanya mazungumzo na Makamu Mwenyekiti wa wamiliki wa Mitumbwi Bibi Stella Sylivester ambaye ameleza masikitiko yake makubwa ya hasara waliyoipata kufuatia tukio hilo na kusema kwa sasa wamebaki maskini kwa kuwa mtaji wao wa mitumbwi na makokoro umeharibiwa na hawana cha kufanya na kuomba kuwe na mpango wa kuwasaidia kwenye majanga kama hayo yaliyowakumba.
Pia Bryson Majura . Meneja Victoria Farming and Fishing Organization (VIFAFIO) ameioambia TMFD kufikisha kwa Serikali kilio chao kikubwa ni kutotambulika kama zilivyo sekta nyingine zinapopatwa na majanga kwani hili lililotokea katika mwalo wa busekera limewaacha wavuvi wakiangaika wenyewe bila kuwa na msaada wowote .
Bwana Soko amesema ni wakati muafaka sasa kwa Serikali kuwa na mpango wa kuwasaidia wavuvi wanapopata majanga kama haya hasa kwa kuona uwezekano wa kuwa na bima kwenye sekta ya uvuvi kwani sekta hiyo inakuwa kwa kasi na inachangia maoato makubwa kwenye uchumi wa Nchi.
"Mwalo wa busekera ni mwalo mkubwa kwa shughuli za uvuvi wa dagaa katika Kanda ya Ziwa hivyo unapoathirika na mapato yanaathirika pia " Alisema Soko
Pia Soko aliongeza kuwa TMFD inajikita kwenye maeneo mbalimbali ya sekta ya uvuvi likiwemo eneo la usalama wa wavuvi na zana zao za uvuvi hivyo lina wajibu mkubwa wa kuibua changamoto zinazoikabili sekta ya uvuvi ili zipate majibu ili kuchochea maendeleo ya sekta ya uvuvi nchini.
0 Comments