Kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Uyui mkoani Tabora, Dkt Kija Maige akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake .
Mganga mkuu wa halmashauri ya wilaya ya Uyui mkoani Tabora ,Dkt Wendy Robert akisisitiza jambo mbele ya waandishi wa habari .
mkuu wa idivisheni ya utawala na usimamizi wa rasilimali watu wilaya ya uyui mkoani Tabora, Hamis Mpume akifafanua sheria za kazi zikiwemo kanuni za utumishi wa umma
Na Lucas Raphael,Tabora
Halmashauri ya wilaya ya Uyui mkoani Tabora amewasimamisha kazi watumishi wawili wa kada ya afya baada ya kutoa lugha zisizofaa wakiwa kazini na kusambazwa katika mitandao ya jamii jambo ambalo ni kinyume na sheria za utumishi wa Umma.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana Kaimu mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya ya Uyui mkoani hapa Dkt Kija Maige alisema kwamba tukio hilo lilitokea januari sita mwaka huu katika zahanati ya Ishilimulwa kata Bukumbi wilayani humo.
Aliwataja watumishi hao kuwa ni Rose Shirima muuguzi mkunga na James Chuchu Mteknolojia wa maabara ambao walikuwa wakibishana na kutoleana lugha zisizofaa kazini hali iliyosababisha taaruki kwa umma.
Dkt Maige alisema watumishi hao watapumzishwa kutekeleza majukumu yao ya utoaji wa huduma za afya ili kupisha Uchunguzi kwa mujibu wa kanuni 37 ya kanuni za utumishi wa umma ya mwaka 2003.
Alisema kwamba uchunguzi huo utashirikisha mabaraza ya kitaaluma ambayo ni baraza la wauguzi Tanzania na baraza la wataalam wa maabara Tanzania ambapo hatua zaidi zitafuata baada ya kukamilika kwa uchunguzi huo.
Aidha mganga mkuu wa halmashauri ya wilaya ya Uyui Dkt Wendy Robert alisema kuwa mabishano hayo yalionekana mtandaoni na kusababisha taharuki kubwa kwa wananchi na kusema tayari uchunguzi umeanza kufanyika ili kujua chanzo cha mabishano hayo.
Alisema mabishano hayo yalitokana na mtaalam wa maabara kugomea kutumia kipimo cha malaria kwa ajili ya kinamama wajawazito kwa madai kilikuwa kimekwisha muda wake kitu jambo si sahihi.
“Vitendanishi hivyo vinamalizika muda wake wa matumizi Aprili 14 mwaka huu jambo ambalo bado kipimo hicho kinafaa kwa ajili ya kupimia wajawazito kujua wingi wa wadudu wa malaria”alisema Dkt Wendy. Alisema kwamba kipimo hicho cha malaria chenye namba ya utambuzi iliyosajiliwa ni 05EDG025B
Naye mkuu wa idivisheni ya utawala na usimamizi wa rasilimali watu wilaya ya uyui Hamis Mpume alisema kuwa watumishi hao watasimama kazi kwa ajili ya kupisha uchunguzi wa tuhuma kwa kuzingatia kanuni na sheria.
Aliwataka watumishi wote wa halmashauri ya wilaya ya uyui kuhakikisha wanazingatia sheria za utumishi na kuepukana na maneno yanayoweza kumuathiri mtumishi wa umma.
Picha na video za watumishi hao zilionekana mitandao wakibishana na kutoleana lugha zisizofaa kazini hali iliyosababisha taharuki kwa umma.
0 Comments