Header Ads Widget

RAIS WA AFRIKA KUSINI CYRIL RAMAPHOSA ACHAGULIWA TENA KUIONGOZA ANC.

Rais wa Afrika Kusini aliyekumbwa na kashfa Cyril Ramaphosa amechaguliwa tena kuwa kiongozi wa chama tawala cha African National Congress (ANC).


Alimshinda mpinzani wake Zweli Mkhize kwa kura 2,476 dhidi ya 1,897. Bw Ramaphosa alishinda licha ya kutawaliwa na madai ya ufujaji wa pesa, na ongezeko la dakika za mwisho la kumuunga mkono Bw Mkhize, ambaye pia amekuwa akishutumiwa kwa ufisadi. Wote wanakanusha madai hayo.


Ushindi wake unamweka katika nafasi nzuri ya kuongoza ANC katika uchaguzi wa 2024.


Lakini bado yuko hatarini kwani anachunguzwa na polisi, ofisi ya ushuru na benki kuu kuhusu madai ya kuficha angalau dola 580,000 kwenye sofa kwenye shamba lake la kibinafsi, na kisha kuficha wizi wake.


Jopo la wataalam wa sheria walioteuliwa na spika wa bunge, walisema kuwa kesi za kumfungulia mashitaka zinapaswa kuanzishwa kwa kuwa anaweza kuwa amekiuka katiba na kuvunja sheria ya kupinga ufisadi. Azma ya Bw Ramaphosa kuchaguliwa tena iliimarishwa na ukweli kwamba ANC ilitumia wingi wake wa wabunge kupigia kura maoni ya jopo hilo.


Rais Ramaphosa amekana kufanya makosa yoyote, na ameanzisha hatua za kisheria kubatilisha ripoti ya jopo hilo. Alisema dola 580,000 zilitokana na mauzo ya nyati, lakini jopo hilo lilisema kulikuwa na "mashaka makubwa" juu ya kama shughuli hiyo ilifanyika.


Bw Mkhize alikuwa waziri wa afya katika serikali ya Bw Ramaphosa, hadi alipolazimika kujiuzulu mwaka jana kwa madai ya matumizi mabaya ya fedha zilizotengwa kukabiliana na janga la Covid-19.


Yeye pia amekana kufanya makosa yoyote, na wafuasi wake waliona madai hayo kama jaribio la kumchafua. Bw Ramaphosa ndiye aliyepewa nafasi kubwa ya kushinda, lakini Bw Mkhize alipata kura nyingi zaidi kuliko ilivyotarajiwa baada ya kutoa nyadhifa muhimu kwa viongozi wengine wenye nguvu katika mikataba iliyofikiwa kabla ya wajumbe kupiga kura kwenye mkutano huo.


Pande zote mbili zilikanusha tuhuma za ununuzi wa kura. Chama cha ANC kimekuwa madarakani tangu utawala wa wazungu wachache kumalizika mwaka 1994, na kinatarajia kupata muhula wa sita katika uchaguzi wa bunge wa 2024.


Lakini kura za maoni zinaonyesha kuwa kura yake imepungua kwa kiasi kikubwa kutokana na kuenea kwa rushwa serikalini, ukosefu mkubwa wa ajira na huduma duni za umma - ikiwa ni pamoja na kukatika kwa umeme kila mara.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



BBC NEWS