Na Mwandishi Wetu, MatukioDaima App
Mkutano Mkuu wa vyama vya Kidemokrasia Barani Afrika (Democrat Union of Africa - DUA) umemchagua Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe kuwa Mwenyekiti Mwenza wa Umoja huo.
Mkutano huo mkuu uliofanyika Jijini Abidjan, Ivory Coast kuanzia Jumapili Novemba 6, na kuhitimishwa jana Novemba 9, 2022 pia ulimchagua Louisa Atta-Agyemang wa chama tawala nchini Ghana, New Patriotic Party - NPP
kama Mwenyekiti Mwenza atakayesaidiana na Mbowe kufanya mageuzi ya kimfumo na utendaji ndani ya DUA ili kukidhi mahitaji ya vyama vya mrengo wa kati barani Afrika.
Taarifa iliyotolewa jijini Abjan na kusambazwa kwenye mitandao ya kijamii jana Novemba 9, 2022 ilisema Mkutano mkuu wa DUA umeamua kuwa na wenyeviti wenza wawili ili kurahisisha utendaji na ufuatiliaji wa mkakati wa kueneza itikadi ya mrengo wa kati barani Afrika.
Taarifa hiyo imesema, wenyeviti wenza wataongoza Bodi ya watu nane itakayojumuisha Makamu wenyeviti kutoka Kanda tano za Afrika ambazo ni Kaskazini (Morocco), Magharibi (Togo/ Nigeria), Kati (Equatorial Guinea) Mashariki (Kenya) na Kusini (Malawi).
"Kikao cha kwanza cha Bodi ya DUA kilichoongozwa na Mbowe kimeamua kuhamisha makao makuu ya Sekretariati ya DUA kutoka Accra Ghana kwenda Afrika ya Kusini" ilisema sehemu ya taarifa hiyo.
Kwa nafasi hiyo Mbowe atakuwa mmoja wa Makamu wenyeviti wa Umoja wa vyama vya Kidemokrasia Duniani- International Democrat Union (IDU) kutokea Afrika.
0 Comments