Header Ads Widget

MAHAKAMA KUU YAWAACHIA HURU MAKADA WA CHADEMA

 

Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Shinyanga imewaachia huru makada wawili wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Katala Kikaja na Ng'hulima Lilanga waliohukumiwa kifungo cha maisha jela kwa makosa ya wizi, unyang'anyi wa kutumia silaha na ubakaji.

 

Uamuzi huo umetolewa leo Jumatano Novemba 16, 2022 na Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga, Athuman Matuma baada ya kuridhika na hoja za warufani kuwa ushahidi uliowatia hatiani Aprili 12, mwaka huu, ulikuwa dhaifu, unaotia mashaka na usiokubalika mbele ya macho ya sheria.

 

Wana Chadema walitiwa hatiani kwa makosa mawili ya wizi, ubakaji, kuharibu mali na unyang’anyi wa kutumia silaha baada ya kukamatwa wakiwa kituo cha kupigia kura Kata ya Dutwa Wilaya ya Bariadi mkoani Simiyu walikokuwa mawakala wa wagombea wa chama hicho kikuu cha upinzani katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 28, 2020.

 

Pamoja na wizi wa Sh300, 000 warufani hao kwa pamoja walidaiwa kumbaka msaidizi wa kituo cha kupigia kura ambaye jina lake lilihifadhiwa kulinda utu na heshima yake mbele ya jamii.

 

Tangu walipokamatwa siku ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 28, 2020, kufikishwa mahakamani na kuhukumiwa kifungo Aprili 12, mwaka huu, warufani hao wamekaa mahabusu na gerezani kwa takribani miaka miwili na miezi mitatu kutokana na shitaka la unyang’anyi wa kutumia silaha ambayo ni moja ya mashtaka yaliyokuwa yanawakabili kutokuwa na dhamana.

 

Hadi kuachiwa huru leo, warufani hao wametumikia takribani miezi saba ya adhabu yao katika magereza ya Bariadi, Shinyanga na Butimba jijini Mwanza.


Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI