Teddy Kilanga , MatukioDaimaAPP Arusha
Katika kuhakikisha wananchi wanashiriki kikamilifu Katika Sensa ya watu na makazi inayotarajiwa kufanyika Agosti ,23,mwaka huu,halmashauri ya jiji la Arusha wamefunga kampeni ya uhamasishaji na utoaji elimu baada ya kuwafikia makundi yote.
Akizungumza Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya jiji la Arusha,Hargney Chitukuro baada ya kufunga mafunzo ya Sensa kwa Chama cha washehereshaji ambapo alisema wamefunga baada ya kuwafikia makundi yote wakiwemo watu wenye ulemavu,wazee,vijana na wanawake.
"Sisi jiji la Arusha tumetumia njia mbalimbali za uelimishaji jamii juu ya Sensa inayofanyika mwaka huu lengo ni wananchi waelewe umuhimu wake na kusiwe na taharuki hata kwa mawakala wetu wanapofika katika makazi ya watu,"alisema Chitukuro.
Aliongeza kuwa hadi sasa wananchi wamepata uelewa wakutosha kwani wamefanya uhamasishaji katika sehemu mbalimbali yenye mikusanyiko pamoja na kutoa mafunzo katika makundi ambayo hayawezi kufikika.
"Pia tumewafikia wafanyabiashara mbali,viongozi wa dini ,watu wenye ulemavu,vijana na wanawake lengo ni ikifika Agosti 23 mwaka huu kila mwananchi aweze kutoa taarifa zao sahihi,"alisema.
Kwa upande wake mmoja wa washehereshaji(MC)Mohamed Msofe alisema chama cha washehereshaji kimekuwa na mwamko wa uhamashaji sensa jamii kwa kushirikiana na serikali kupitia kazi zao za kukutana na kundi kubwa la wananchi.
Aidha Msofe alisema Sensa ni muhimu katika jamii na Taifa kwa ujumla kwani itasaidia serikali kuweka bajeti ya maendeleo katika maeneo mbalimbali kulingana na uhitaji wa watu katika maeneo husika.
"Sensa itasaidia kusogeza huduma muhimu kwa wananchi kulingana na mahitaji ya watu katika maeneo husika na ndio maana mawakala watakaopita katika makazi ya watu wanahitaji taarifa sahihi hivyo ni vyema wananchi wakatoa ushirikiano mzuri ili kuweza kufanikisha,"alisema.
0 Comments