Licha ya Sera ya Afya kuelekeza kila Kijiji lazima kiwe na Zahanati lakini bado wakazi Zaidi ya 5000 wa kata ya Navanga Halmashauri ya Mtama Mkoani Lindi wamejikuta wakitembea umbali mrefu wa Takribani kilometa tisa kufuata huduma hiyo hali inayopelekea akina mama kujifungulia njiani .MWANDISHI HADIJA OMARY MDTV LINDI
Pamoja na kwamba wataalamu wa Afya wanasisitiza kuwa ni muhimu kwa mama anapohisi tu mjamzito kuhudhulia kliniki ili kuweza kupata chanjo na ushauri lakini hali hiyo ni tofauti kwa akina mama wa Navanga ushindwa kufanya hivyo kutokana na gharama kubwa ya usafiri wanazotumia wakati wakifuata huduma hizo
Akizungumza na Mtukio Daima Issa Chande Mkazi wa Navanga alisema kuwa kutokuwepo kwa huduma hiyo Afya katika maeneo yao kunapelekea akina mama kushindwa kuhudhuria kliniki kwa wakati pindi wanapokuwa wajawazito na wengine kujifungulia njiani wakiwa wanafuata huduma hiyo
“ tuna miaka mingi hatuna Hospitali Navanga, huduma inakopatikani ni Nachunyu mimi mwenyewe ninaezungumza mke wangu aliwahi kuwa na Ujauzito aliwahi kujifungulia njiani wakati tunaelekea kwenye hiko Kijiji cha jirani hata hivyo kulingana na huduma alizohitaji tulilazimika kutoka katika hospitali hiyo ya Nachunyu kwenda Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Lindi Sokoine kwa ajili ya Matibabu Zaidi”
Nae Ashura Salamu Mkazi wa Navanga alisema kwa kuwa huduma za Afya zinapatikana mbali na maeneo yao ulazimika kutumia sio chini ya shilingi elfu 5000 kama nauli ili kuzifikia huduma hizo jambo ambalo kwa Maisha ya sasa inakuwa ni ngumu.
“uwe na hela ya kulipia nauli , uwe na hela ya kulipia huduma na hali ya sasa ilivyokuwa ngumu tunashindwa . utakuta mtu anaenda kuanza kliniki miezi michache ya mwishoni au asiende kabisa jambo ambalo ni hatari kwa afya ya mama na mtoto alie tumboni”
Kwa upande wake Diwani wa kata hiyo Rashidi Mkuya alisema kuwa kwa kutambua changamoto wanazokabiliana nazo wakazi wa kata hiyo hasa katika vijiji vya Navanga, Nampunga na Mongo Mongo wananchi wenyewe wameona ipo haja ya kujitolea kwa nguvu zao kwa ajili ya kuanzisha ujenzi wa Zahanati katika Kijiji Cha Navanga ambayo itakuwa katikati ya vijiji hivyo ambavyo vimekosa huduma za Afya ambao kwa sasa umefikia hatua ya boma la kozi kumi
Kwa upande wake Mganga Mkuu Wa Halmashauri ya Mtama DKT, Dismas Masulumbu amekili kuwepo kwa changamoto hiyo ambapo alisema kuwa kata ya Navanga ni miongoni mwa vijiji vitano vilivyopo katika halmashauri hiyo ya Mtama ambavyo Wananchi wenyewe kwa kutambua umuhimu wa huduma za Afya wameanzisha ujenzi wa Zahanati ambao umefikia katika hatua mbali mbali za umaliziaji
Alivitaja vijiji hivyo kuwa ni pamoja na Navanga, Nauka uka A, Nauka uka B, Ruhokwe na Ntene ambayo mpaka sasa wanasubiri fedha kutoka Serikali kuu kwa ajili ya umaliziaji ambao utafanywa kwa kipaumbele kulingana na hatua ya jingo ilipofikia
Hata hivyo pamoja na kuwapongeza Wananchi wa maeneo hayo kwa jitihada walizozionyesha za kuanzisha ujenzi huo wa zahanati pia alitoa wito kwa wananchi hao kuendelea kushirikiana katika kuendeleza ujenzi huo ili uweze kusogea mbele Zaidi
Hata hivyo kwa kutambua umuhimu wa Zahanati hiyo kupitia Mkutano wa Mfuko wa jimbo wenye lengo la kugawa fedha za maendeleo kwenda kuchochea shughuli mbali mbali kilichoongozwa na Mbunge wa Jimbo hilo , Waziri wa Habari Mawasiliano na teknolojia ya Habari Nape Nnauye umetenga jumla ya shilingi milioni tatu kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa Zahanati hiyo
Ili Mtoto aweze kukua vizuri swala la Afya kabla na baada ya kuzaliwa ni miongoni mwa mambo matano muhimu yaliyotajwa kwenye Program jumuishi ya Taifa ya malezi makuzi na maendeleo ya awali yam toto (PJT-MMMAM)
0 Comments