Header Ads Widget

WAZIRI MKUU AKUTANA NA KUFANYA MAZUNGUMZO NA SANJAY DATT

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amekutana na kufanya mazungumzo na muigizaji mashuhuri wa filamu za Kihindi kutoka nchini India, Sanjay Dutt ambaye ameahidi kushirikiana na Serikali katika kukuza tasnia ya filamu nchini.

Alikutana na msanii huyo jana (Jumatano, Novemba 10, 2021) katika ofisi ndogo ya Waziri Mkuu Magogoni jijini Dar es Salaam. Waziri Mkuu alisema Serikali itampa ushirikiano wote kuhakikisha msanii huyo anatimiza malengo ya ziara yake nchini.

 

Majaliwa alitumia fursa hiyo kuwataka wadau wa filamu nchini kutumia ujio wa msanii huyo mkubwa duniani kuimarisha uhusiano pamoja na kujifunza namna bora ya kuboresha kazi zao kupitia yeye na kuweka mipango ya kufanyakazi kwa pamoja.

 

Pia, Waziri Mkuu alimshukuru msanii huyo ambaye pamoja na mambo mengine ameahidi kushirikiana na Bodi ya Filamu Tanzania katika kuendesha mafunzo ya masuala mbalimbali katika tasnia  hiyo  ikiwemo uandaaji wa filamu kwa kutumia teknolojia ya kisasa hususani kwa vijana.

 

Naye, Dutt alisema amevutiwa na fursa nyingi zilizoko kwenye sekta ya utalii nchini na kwamba ameahidi kuvitangaza vivutio hivyo na kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa kwenye ramani ya dunia katika masuala ya utalii.

 

Mbali na ahadi hiyo, pia msanii huyo alisema atashirikiana na wadau wa filamu nchini wakiwemo waandaaji pamoja na waigizaji kutoa mafunzo na mbinu bora zitakazowawezesha kuboresha kazi zao na hatimaye waweze kupata mafanikio zaidi.

 

Alisema kuwa katika ziara yake anatarajia kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii ambapo atapiga picha kwa ajili ya kuvitangaza ili kuwavutia watu wengi waje Tanzania. Miongoni mwa vivutio hivyo ni pamoja na mbuga ya wanyama za Serengeti na Ngorongoro.

 

"Jana nilikuwa Zanzibar nimeona fursa nyingi za uwekezaji hapa Tanzania ikiwemo uwepo wa fukwe nzuri. Nitakwenda kuwashawishi marafiki zangu nao waje kuwekeza. Naipenda sana Tanzania watu wake ni wakarimu na ninatarajia kuja kufanya filamu."

 

Wakati huo huo, Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo Innocent Bashungwa alisema kupitia ujio wa Dutt, Wizara inategemea kuangalia maeneo ya kimkakati ambayo wanaweza kushirikiana na msanii huyo ikiwemo uandaaji wa filamu, kuongeza wigo wa masoko ya filamu na matumizi ya teknolojia katika kuikuza sekta ya filamu nchini.

 

Aliongeza kuwa kupitia Chuo cha Sanaa Tanzania (TaSUBa) Dutt alitoa ushauri wa namna bora ya kushirikina ikiwemo kutoa mafunzo kwa wasanii na waandaaji  wa filamu “Lengo letu ni kuhakikisha wasanii wetu wanatengeneza filamu ambazo zitakuwa na viwango vya kimataifa na ameahidi kuwaleta wataalamu ili wawasaidie wasanii wetu”

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI