Aliyekuwa
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Christian Makonda, anatarajiwa kufikishwa
mahakamani, wakati wowote kuanzia sasa.
Makonda anatarajiwa
kufikishwa mahakamani, pamoja na mambo mengine, kujibu tuhuma za matumizi
mabaya ya madaraka ikiwemo kuvamia kituo cha televisheni cha Clouds Media, Dar
es Salaam.
‘’nakwambia
hivi, mchakato wa kumfikisha Makonda mahakamani, tayari umeiva. Muda wowote
wiki hii, kesi yaweza kufunguliwa nay eye kupelekewa mwito wa kutakiwa kuja
kujitetea,’’ anaeleza mmoja wa mawakili ambaye amepewa jukumu la kufungua
shauri hilo.
Kupatikana
kwa taarifa kuwa Makonda yuko hatarini kufikishwa mahakamani, kunakuja huku
Mkuu wa Wilaya ya Hai, Kilimanjaro, Lengai ole Sabaya akitumikia kifungo cha
miaka 30 gerezani.
Sabaya na
wenzake watatu walihukumiwa kifungo hicho na Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha
mwezi uliopita baada ya kupatikana na hatia ya wizi na unyang’anyi wa kutumia
silaha.
Aidha,
Sabaya na wenzake sita wanakabiliwa na mashtaka mengine kadhaa, ikiwamo
kuendesha genge la uhalifu, uhujumu uchumi, utakasishaji fedha na matumizi
mabaya ya madaraka.
Wote wawili
Sabaya na Makonda waliteuliwa kushika nyadhifa zao na Rais John Magufuli ambaye
alifariki dunia Machi 17 mwaka huu.
Miezi miwili
baadaye, Rais Samia Suluhu Hassan aliyemrithi Magufuli akatangaza kumsimamisha
kazi Sabaya ambaye aliwahi pia kuwa Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha
Mapinduzi(UV-CCM), Mkoa wa Arusha, ili kupisha uchunguzi wa tuhuma zilizokuwa
zikimkabili.
Baadhi ya
wachambuzi wa kisiasa na utawala bora, wanawataja Sabaya na Makonda kuwa mfano
wa viongozi wababe waliovunja sheria na kwenda kinyume na maadili ya kazi zao
lakini walikuwa hawaguswi kwa madai kwamba walilindwa na mamlaka zao za uteuzi.
Kwa mujibu
wa maombi yaliyopo, Makonda anadaiwa kuvamia kituo hicho cha televisheni cha
Clouds na kuingilia maudhui ya kipindi cha Shilawadu, Machi 17, 2017.
Mashtaka
dhidi ya Makonda yanafunguliwa na Mwanasheria wa kujitegemea anayefanyia
shughuli zake Dar es Salaam. Mwanasheria huyo ameomba kibali cha Mahakama
kumshtakiMakonda kutokana na makosa anayodaiwa kuyatenda wakati akiwa Mkuu wa
Mkoa wa Dar es Salaam kinyume cha sheria namba 96.
Makonda anadaiwa
kuwa siku hiyo ya Machi 17, 2017 saa 3;40 usiku katika ofisi za Clouds
Mikocheni akiwa na watu wengine wanaoaminika kuwa ni walinzi wake, alivamia
kituo hicho cha utangazaji
Kwamba siku
hiyo Makonda na kundi lake walimfuata mtangazaji wa kipindi cha Shilawadu na
kumlazimisha arushe video inayomwonesha mwanamke aliyejulikana kwa jina la
Grace Athuman, ambaye anadaiwa kuwa na uhusiano wa kimapenzi na Askofu wa
Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima kinyume cha taratibu na kanuni
walizojiwekea katika kazi zao.
Video hiyo
ambayo haijulikani ilirekodiwa wapi na nani, inadaiwa kumwonesha Grace akieleza
kwa undani uhusiano wake na Askofu Gwajima, hali ambayo ingeweza kuchafua jina
na heshima ya kiongozi huyo wa kiroho na familia yake.
Ikumbukwe
kuwa wakati Makonda anavamia Clouds na kulazimisha kurushwa kipindi hicho,
alikuwa na vita vya maneno na Askofu Gwajima. Kwa mujibu wa hati hiyo ya
mashitaka, kosa la pili ambalo Makonda anakusudiwa kuburuzwa nalo kortini ni
kuingilia maudhui ya matangazo ya Clouds kinyume na sheria.
Katika maombi
hayo mlalamikaji ameambatanisha taarifa ya Kamati iliyoundwa na aliyekuwa
Waziri wa Michezo, Nape Nnauye. Taarifa ya Nape iliyotaka Makonda achukuliwe
hatua za kiwajibikaji na mamlaka yake ya uteuzi haikufanyiwa kazi, kwani muda
mfupi baada ya kusoma sehemu ya ripoti hiyo mbele ya waandishi wa habari, Rais
Magufuli alitengua uteuzi wake.
Baadhi ya
wajumbe wa Kamati hiyo ni Deodatus Balile ambaye sasa ni Mwenyekiti wa Jukwaa
la Wahariri Tanzania (TEF), aliyekuwa Mhariri Mtendaji wa The Guardian, Jesse
Kwayu na Mkurugenzi wa Upendo Radio, Neng’da Johanes. Wengine ni Mabel Masasi,
wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) na Dk Hassan Abbas ambaye wakati huo
alikuwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari(Maelezo na Msemaji Mkuu wa Serikali).
Kwa mujibu
wa ripoti hiyo, pamoja na Kamati hiyo kujitahidi kumtafuta Makonda kwa ajili ya
mahojiano, kiongozi huyo alikataaa katakata kufika mbele yake.
Matokeo ya Kamati
Kamati hiyo
ilithibitisha kuwa Makonda alivamia kituo cha Clouds saa nne usiku, akiwa anaendesha
mwenyewe gari namba T553BFM.
Kamera za
CCTV na kitabu cha kumbukumbu za walinzi kilionesha kuwa Makonda aliingia akiwa
na askari wane waliokuwa na sare tofauti za majeshi ya ulinzi na usalama, kati
yao watatu wakiwa na silaha za moto.
Pia kamati
hiyo imethibitisha kuwa Makonda na askari wake waliingia hadi chumba cha
utangazaji jambo ambalo ni kinyume na kanuni za utangazaji.
Ripoti hiyo
ilibainisha kuwa katika hatua hiyo ambayo ni kinyume cha sheria, Makonda
alitumia vitisho dhidi ya wafanyakazi wa Clouds kwa kutumia silaha za moto. Aidha,
Kamati hiyo ilibainikuwepo uvunjaji wa sheria ya habari ya mwaka 2016 kwa
kitendo cha kuingilia uhuru wa uhariri na vyombo vya habari kwa kiwango cha juu
kutokana na vitisho na amri alizotoa.
Maoni ya
Kamati yalibaini kuwa vitendo vya Makonda vinaashiria uvunjifu wa sheria za
nchi, hususani zinazohusu utangazaji na huduma ya habari.
Kamati ilibaini
dalili za Makonda kutotambua ukubwa wa madaraka aliyonayo na kujikuta
anayatumia vibaya katika mazingira yasiyostahili.
Pia kamati
ilibaini kuwa uongozi wa Clouds ulistahili pongezi kwa kusimamia misingi,
sheria na maadili ya uandishi wa habari kwa kukataa kurusha habari isiyo na
mizania.
Mapendekezo
ya Kamati hiyo yalimtaka Makonda awaombe radhi wafanyakazi wa Clouds na vyombo
vya habari nchini kwa tukio hilo la ukiukwaji wa usalama na maadili ya uandishi
wa habari.
Aidha,
kamati ilipendekeza aliyekuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
wakati huo Nape awasilishe ripoti hiyo kwa mamlaka ya uteuzi ili ichukue hatua
stahiki.
Mapendekezo
mengine yalikuwa ni kuvitaka vyombo vya Dola kuanzia uchunguzi dhidi ya askari
walioingia kwenye chumba cha habari na silaha za moto ili kuzuia matukio kama
hayo kutokea wakati mwingine.
Kamati ilipendekeza kwa Clouds Media kupitia miongozo, kanuni na sheria zinazoongoza shughuli za utangazaji na kuangalia njia bora ya kuwa na udhibiti kwa watu wasiohusika kuzoea kuingia mara kwa mara na kufanya kazi za uhariri bila wanataaluma wa habari au wahusika katika chumba cha habari.





0 Comments