Header Ads Widget

MADIWANI WAIOMBA TUME YA MAWAZIRI KUFIKA KILIMANJARO

Diwani wa kata ya Kata ya katangara Mrere katika halmashauri ya wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro Venance Malleli amefikisha hoja binafsi katika kikao cha baraza la madiwani wa halmashauri hiyo akiitaka serikali kuleta  tume ya mawaziri nane(8) ili kusuluhisha migogoro ya mipaka iliyopo baina ya hifadhi ya mlima Kilimanjaro(KINAPA) na wananchi waishio vijiji vya jirani. mwandishi wa matukio daima Gift Mongi anaripoti kutokea Kilimanjaro

Diwani huyo alisema kuwa  mamlaka ya hifadhi ya mlima Kilimanjaro(KINAPA)imepakana na vijiji 19 vya halmashauri ya Rombo ambavyo vimetenganishwa  na eneo la msitu wa nusu maili(half mile) linalosimamiwa na halmshauri za wilaya zinazozunguka Mlima Kilimanjaro.

"Mheshimiwa mwenyekiti naomba ikumbukwe kuwa mwaka 2005 serikali ilibadilisha usimamizi kutoka  halmashauri bila  kuwashirikisha wananchi kutoka katika vijiji vinavyoizunguka hifadhi na hapa ndipo migogoro ilipoanzia"alisema Mallel

Katika hoja hiyo Mallel alisema baada ya  hifadhi ya KINAPA  kupewa usimamizi wa eneo la msitu la (half mile) 2005 kumekuwepo na migogoro mingi baina ya wananchi na maafisa wa hifadhi ya mlima Kilimanjaro ambapo baadhi ya wananchi wameripoti vitendo vya  unyanyasaji,kupigwa kubambikiwa kesi kwa kubebeshwa magogo ya miti mibichi, pia wananchi ambao hukata majani ya malisho ya mifugo hukamatwa na kusafirishwa  umbali mrefu kutoka wilaya ya Rombo hadi katika wilaya ya Moshi(manispaa) kwa ajili ya kufunguliwa mashtaka  wakati vituo vya polisi pamoja na mahakama vinapatikana ndani ya wilaya ya Rombo na ni wilaya kamili yenye mipaka  na utawala wake halali wa kisheria

Alisema kuwa  idadi ya wananchi wa halmashauri ya Rombo na wilaya jirani na hifadhi imeongezeka  hivyo kuongeza mahitaji ya wananchi yakiwemo kuni kavu kwa ajili ya kupikia  malisho ya mifugo hususani kwa familia nyingi zinazoishi kipato cha chini ipo haja sasa kuangaliwa kwa suala hilo kwa mapana zaidi

"Mwaka 2020 pale katika chuo kikuu cha ushirika mjini Moshi,pamoja na katika eneo la Njiapanda ya Mji mdogo wa Himo serikali ya awamu ya tano chini ya hayati Dkt John Pombe Magufuli ilituahidi endapo itachaguliwa na kuingia madarakani itahakikisha kuwa eneo la nusu mile litarejeshwa kwenye usimamizi wa halmashauri zinazozunguka mlima Kilimanjaro hivyo ni muda muafaka kwa sasa ahadi hii iende kutekelezwa"alisema

Hata hivyo diwani huyo alilitaka baraza hilo kurejea  kauli ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan aliyoitoa  tarehe 15.10.2021 katika uwanja wa chuo kikuu cha ushirika cha mjini Moshi ambapo aliahidi suala la Nusu maili litashughulikiwa na serikali

"Naomba azimio la baraza lako tukufu kuiomba serikali kutuletea tume maalum ya rais inayoongozwa na Wilium Lukuvi waziri wa ardhi ili wafike katika wilaya  ya Rombo kusuluhisha migogoro iliyopo baina ya wananchi na mamlaka ya hifadhi ya mlima Kilimanjaro(KINAPA) kama ilivyosuluhisha katika hifadhi nyingine zikiwemo Serengeti na Ngorongoro"alisema

Akiunga mkono hoja hiyo diwani wa kata ya Kitirima Amedeus Mrema aliiomba timu hiyo ya mawaziri kuja Rombo kwa ajili ya utatuzi maana wananchi wananyanyasika sana kutokana na hali ya kiuchumi kuzidi kushuka  ambapo jamii inategemea nyasi kwa ajili ya malisho ya mifugo.

Diwani wa  Ubetu Obrey Mrema alisisitiza umuhimu wa hao mawaziri kuja ili kuweza kumsadia rais kutatua mgogoro kwani jamii ya pale haina tena ujirani mwema na watu wa hifadhi kutokana na manyanyaso wanayoyapata kutoka miongoni mwa skari wa hifadhi kuwakata na kuwabambikizia kesi kubwa.

"Kitendo cha askari wa KINAPA huwakamata hadi wamama wa  miaka 70 na kuwasafirisha  kwa usiri hadi Moshi bila kuwataarifu ndugu ni ukatili mkubwa na wa hali ya juu na kuwa kuna mtu alitumia wiki kumtafuta mama yake akidhani amepotea kumbe alimakatwa na kusafirishwa hadi kituo cha polisi Majengo Moshi"alisema Athumani Kimario diwani wa Mrao Keryo

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI