Wajibu wa kampuni katika jamii ni haki ya kampuni kuzingatia maadili na kuchangia katika maendeleo ya kiuchumi wakati huohuo ikiboresha maisha ya wafanyakazi na familia zao ikiwa ni pamoja na jamii za wenyeji na wanajumuia kwa ujumla wake. mwandishi wa matukio daima Gift Mongi anaripoti kutokea Moshi
Tangu kuanza kwa uchumi wa soko huria, uliotokana na mabadiliko ya mfumo wa uchumi duniani katika miaka ya 1980 kumekuwepo na ongezeko la kasi la makampuni mengi ya kitaifa na kimataifa hapa nchini kwa miaka kadhaa hivi sasa
Kutokana na hali hiyo Tanzania ililazimika kubadili sera na sheria zake za kiuchumi ili kuweza kwenda sambamba na mabadiliko hayo ya kiushindani kama ilivyo kwa maeneo mbali mbali duniani ili kuleta usawa katika dhana ya uwekezaji.
Kati ya mwaka 1990 na 2009 zaidi ya sheria 25 zilitungwa kwa lengo la kushughulikia masuala yote yanayotokana na mfumo mpya wa soko huria bila kuathiri upande wowote ule yaani kwa mwekezaji au wazawa.
Madhara yatokanayo na ukosefu wa ukiukwaji wa sheria za kusimamia makampuni/ viwanda kuwajibika kwa jamii ni mengi na yamekuwa yakijidhihirisha katika maeneo mbalimbali nchini ingawa kwa sasa yanaonekana kupungua kutokana na uelewa uliojengeka
Miongoni mwa mambo hayo ni pamoja na uchafuzi wa mazingira unaotokana na shughuli mbalimbali za makampuni hususani zile sehemu zenye uchimbaji wa madini na viwanda vikubwa ingawa si vyote.
Kukithiri kwa migogoro ya ardhi hususani pale kampuni zinapora ardhi ya wazawa na kuwaacha wakiteseka. Ukiukwaji wa haki za binadamu mfano haki ya kuishi, haki ya kutembea na nyingine nyingi.
Kutoa sehemu ya faida ya kampuni kupitia jamii haipaswi kuchukuliwa kama msaada bali ni makubaliano yanayosainishwa kwenye mkataba hivyo ni jambo ambalo lipo wazi na linafahamika ipasavyo .
Kama sehemu ya uwajibikaji kampuni inaweza kurudisha sehemu ya faida yake kwa jamii kwa njia mbalimbali kama vile kutoa michango katika shughuli za kimaendeleo, kutoa mchango katika huduma za afya, kusaidia miundombinu ya usafiri kuhifadhi mazingira kutoa gawio kwa kijiji husika, na kuendeleza hadi kupitia faida.
Katika kudhihirisha hilo kiwanda Cha kuzalisha sukari cha TPC cha mjini Moshi kinakusudia kujenga majengo kwa ajili ya shule ya sekondari eneo la Katanini katika kata ya Karanga lengo likiwa ni kupunguza msongamano wa wanafunzi katika shule ya sekondari TPC.
Ofisa mtendaji mkuu wa Utawala wa TPC Jaffary Ally alisema shule ya sekondari TPC imekuwa ikipokea wanafunzi wengi hivyo ili kupunguza msongamano huo njia itakayotumika ni pamoja na kujenga majengo ya sekondari katika eneo la Katanini.
"Tunajipanga kujenga majengo ya sekondari pale Katanini lengo ni kupunguza msongamano kwenye hii sekondari ya TPC lakini kuondoa adha kwa wale ambao hutembea umbali mrefu kufuata masomo kwani njiani Kuna vitu vingine"alisema
Jaffary alisema kinachosubiriwa kwa hivi Sasa ni mamlaka husika, kama madiwani, ofisi ya elimu na ngazi ya kijiji kukaa na na kuwapatia eneo ili waweze kuanza kwa ujenzi huo mara moja ambao utakua ni mchango tosha kwa jamii inayowazunguka.
"Tunasubiria mamlaka mbali mbali kuanzia ngazi ya kijiji,halmashauri idara ya elimu wenyewe hivyo kila mmoja wakishajidhirisha kuwa ni sehemu sahihi basi sisi tunapewa eneo na kuanza kazi mara moja ya ujenzi huo"alisema
Kwa mujibu wa Jaffary ni kuwa TPC wamekuwa wakisaidia jamii inayowazunguka kwa michango mbali mbali ikiwemo kwenye sekta ya elimu maji ,barabara ,afya na kuwa kwa sasa licha ya kuwa wanaendelea kuchangia ujenzi wa bweni katika sekondari ya TPC bado wanafanya ujenzi huo.
Leonard Waziri ni diwani wa Arusha chini ambapo alisema kwa sasa shule ya sekondari TPC inaendelea na ujenzi wa bweni lenye uwezo wakulaza wanafunzi 80 kwa wakati mmoja na kuwa kukamilika kwake itakuwa ni sehemu salama kwa watoto wa kike ambao hutembea umbali mrefu.
"Wapo watoto wa kike ambao hutembea umbali mrefu Sana kuja hapa ila tunaendelea na huu ujenzi na kuwa TPC wametuahidi kukamilisha na itakuwa imeturahisishia Sana kwa watoto wa kike ambao hukumbana na vishawishi njiani"alisema
Joram Mshiu mkazi wa Moshi alisema wawekezaji wengi hawana budi kurudisha faida wanayoipata kwa jamii kama wanavyofanya TPC kwani jamii inaweza kunufaika kwa uwepo wao kwenye eneo husika tofauti na kama wasingekuwepo.
"Tunashukuru tunaposikia habari njema kutoka kwa wadau Kama wanavyofanya TPC hii ni dhahiri kuwa wanaenda kutatua kero ambazo zimetusumbua kwa kipindi kirefu"alisema
Janeth Malle alisema kiwanda hicho kimekuwa kikisaidia jamii inayoizunguka Kama katika miradi ya afya, maji, ajira na hata nishati na kuwa uwekezaji wao katika eneo hilo umekuwa na tija.
"Mambo mengi yamefanywa na kiwanda hiki kama sehemu ya kurudisha faida kwa jamii na hata muonekano wa shule ya sekondari TPC ilivyo kwa Sasa ni wao wenyewe wamejenga kwa kutusaidia sisi wakazi tunaokizunguka kiwanda hicho"alisema
0 Comments