Header Ads Widget

WAZIRI MAKAMBA AKUTANA NA MAKAMU WA RAIS EQUINOR - AFRICA

Waziri wa Nishati Mh. January Yusuf Makamba amekutana na kufanya

mazungumzo na Makamu wa Rais wa kampuni ya utafutaji na uzalishaji wa

mafuta na gesi asilia ya Equinor (Afrika) Bw. Paul McCafferty.


Viongozi hao wamekutana Oktoba 21, 2021 katika ofisi ndogo za Wizara ya

Nishati zilizopo jijini Dar es Salaam. Mazungumzo hayo yamehudhuriwa pia na

viongozi wengine wa Equinor na Shirika la Maendeleo ya Petroli nchini (TPDC).


Imeelezwa kuwa mazungumzo hayo ni sehemu ya maandalizi ya majadiliano ya

Mkataba wa Nchi Hodhi (HGA) wa Mradi wa Kuchakata na Kusindika Gesi Asilia

(LNG) yanayotarajiwa kuanza rasmi Novemba 8, 2021.


Kwenye kikao hicho, Bw. McCafferty amempongeza Waziri Makamba kwa niaba

ya serikali kwa hatua hiyo ya kuanza tena kwa majadiliano ya mkataba huo wa

HGA kwani yatafungua njia kwaajili ya kuanza kwa utekelezaji wa mradi huo wa

LNG.


Bw. McCafferty ameeleza kuwa Equinor iko tayari kwa majadiliano hayo na

kuongeza kwamba mradi huo ni moja ya miradi yenye uwekezaji mkubwa

inayotekelezwa na Equinor duniani, hivyo ni majadiliano muhimu katika kuweka

msingi mzuri wa utekelezaji wake.

Equinor ni moja ya wabia wakuu wa utekelezaji wa mradi huu wa LNG ambao

utasimamiwa na Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA). Wabia

wengine ni pamoja na kampuni ya Shell na TPDC kwa niaba ya serikali.

Mradi wa LNG unakadiriwa kuwa wa thamani ya takriban Dola za Marekani bilioni

30 huku ukitarajiwa kutengeneza nafasi za ajira za moja kwa moja 6,000 na zisizo

za moja kwa moja zaidi ya 15,000 kwa Watanzania.

Waziri wa Nishati Mh. January Yusuf Makamba, (Wa tatu kutoka kulia) akiwa katika

picha ya pamoja na Makamu wa Rais wa Equinor (Afrika) Bw. Paul

McCafferty, Makamu wa Rais na Mwenyekiti Mkazi, Equinor Tanzania AS, Unni

Merethe Skolstad Fjaer (kushoto kwa Waziri Makamba) na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika

la Maendeleo ya Petroli (TPDC) Dkt. James Mataragio, mara baada ya kikao kifupi

kilichofanyika Oktoba 21, 2021 katika ofisi ndogo za Wizara ya Nishati jijini Dar es

Salaam.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI