Na Fadhili Abdallah,Kigoma
Mgombea ubunge wa jimbo la Kigoma Mjini kwa tiketi ya Chama cha ACT Wazalendo Zitto Kabwe amewataka wapiga kura katika jimbo hilo kumpa kura nyingi za ndiyo katika uchaguzi Mkuu Oktoba 29 mwaka huu aweze kurudi bungeni kuwatumikia lakini pia kulinda heshima ya bunge hilo.
Kabwe alisema hayo wakati wa uzinduzi wa kampeni ya ubunge wa jimbo hilo kwa tiketi ya ACT Wazalendo uzinduzi uliofanyika kwenye Uwanja wa Mwami Luyagwa Gungu Mjini Kigoma ambapo alisema kuwa miaka mitano hii heshima ya bunge imeshuka kwa kutokuwepo kwa wabunge wanaojenga hoja kutetea maslahi ya wananchi.
Mgombea huyo alisema kuwa serikali imekuwa ikipata fedha nyingi kutoka nje kwa kuleta wawekezaji lakini hakuna usimamizi thabiti wa fedha hizo wala wabunge wanaoweza kuikemea serikali kwa matumizi yasiyozingatia nidhamu ya fedha yanayofanyika hivyo hii ni nafasi yake sasa kurudi na kusimamia yale aliyokuwa akisimamia kwa miaka mitano aliyokuwa mbunge katika bunge la Tanzania.
Awali Mwenyekiti wa ACT mkoa Kigoma, Kiza Mayeye alisema kuwa wapiga kura wa jimbo hilo wanahitaji kupeleka bungeni wagombea wanaoweza kusimamia maslahi mapana ya wananchi na kujua jukumu alilonalo badala ya kwenda kuchekesha na kupiga makofi hivyo kuwaomba wapiga kura hao kumchagua Zitto Kabwe.
Naye Mwenyekiti wa ngome ya vijana Taifa ACT Wazalendo, Abdul Nondo alissm juwa kila mtu anao umahiri kwenye eneo lake hivyo ametaka umahiri kwenye mambo ya siasa na kujenga hoja bungeni aachiwe Zitto Kabwe na wale wenye umahiri kwenye Sanaa na burudani kama Revocauts Tryphone Chipando (Baba Levo) wasimamie eneo hilo kwa kuwaburudisha wananchi.
0 Comments