Header Ads Widget

WATU SABA WAKAMATWA KWA TUHUMA ZA MAUAJI YA MFANYABIASHARA WA NYAMA MOROGORO, MWILI WAKE WAOKOTWA TANGA


Watu saba wakiwemo wafanyabiashara wa nyama mjini Morogoro na wengi wao wakiwa ni wakazi wa Mkundi wamekamatwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kufanya mauaji ya kikatili ya mfanyabiashara mwenzao Bernad Masaka, mkazi wa Mkundi, ambaye mwili wake ulikutwa umetupwa kijiji cha Manga, Wilaya ya Handeni mkoani Tanga.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, SACP Alex Mkama amesema watuhumiwa hao waliokamatwa ni Stanley Ng’ambi maarufu Jaha (31), Japhet Michael (29), Yusuph Mkamba (27), Nickson Ibrahim (43), Robson Rite (47), na Ernest Charles maarufu Chief (37), wote wakiwa na makazi Morogoro na Dar es Salaam.


Mmoja wa wafanyabiashara waliokamatwa , Stanley anadaiwa kumrubuni mfanyabiashara huyo kwenda eneo la Makunganya kufuata ng'ombe na badala yake wakamuua na kwenda kuutupa  mwili wake Mkoani Tanga ambapo ulizikwa na halmashauri kwa kukosa ndugu baada ya kuokotwa, lakini upelekezi wa Polisi na vyombo vingine vya kiusalama, na baada ya kuwabana watuhumiwa, walifanikisha kufika eneo la tukio na kuufukua mwili huo na kuuchukua.


Inadaiwa kuwa mnamo Juni 1, 2025, marehemu alitekwa na kuuawa kwa kutumia vitu vyenye ncha kali baada ya kulaghaiwa kuwa anapelekwa Makunganya kununua ng’ombe. Baadaye mwili wake ulipelekwa na kutupwa mkoani Tanga.

Kamanda Mkama amesema uchunguzi wa awali unaonyesha tukio hilo lilitokana na wivu wa kibiashara.

Mwandishi wa matukio Daima alifika usiku Julai 02 mwaka huu,nyumbani kwa marehemu eneo la Mkundi na kushuhudia waombolezaji wakiwa wamekusanyika huku mwili wa marehemu ukiwa umehifadhiwa ndani ya basi dogo aina ya Costa. 

Hata hivyo, waombolezaji na ndugu waligoma kuzungumza na vyombo vya habari.

Mwili huo uliondolewa majira ya saa 2.49  usiku kwenda Matumbulu, mkoani Dodoma kwa taratibu zaidi za maziko.

Wafanyabiashara wenzake wamesema kwa tahadhari kuwa Bernad alikuwa mtu wa nidhamu, aliyejitolea kulinda maslahi ya biashara halali ya nyama sokoni.

 “Alikuwa zaidi ya askari polisi, alikuwa na uthubutu wa kusimamia uadilifu sokoni,” alisema mmoja wao.

Taarifa za ndani zinadai dereva mmoja aliyehusika na usafirishaji wa marehemu ndiye aliyefichua siri ya mauaji hayo baada ya kukamatwa na Polisi, ingawa alikataa kuelekeza eneo halisi la kutupwa mwili kwa madai aliyekwenda kuutupa mwili alikuwa bosi wake baada ya yeye kukataa na kulitelekeza gari.


Marehemu alikuwa mstari wa mbele kupambana na uingizwaji wa nyama isiyo rasmi sokoni na alifahamika kama kiongozi makini katika biashara hiyo,” alisema

Wakizungumza kwa masikitiko baadhi ya wananchi nje ya eneo la msiba akiwemo Adam Chigwa na Rajab Juma walitaka Serikali ichukue hatua kali kwa wote waliopanga na kutekeleza tukio hilo.

Inaelezwa kuwa baada ya kuokotwa Tanga na kukosekana kwa ndugu, mwili wa Bernad ulizikwa huko kabla ya kufukuliwa na kuletwa Morogoro  nyumbani kwake. Mkundi na baadaye kusafirishwa usiku kuelekea Dodoma kwa maziko  baada ya Polisi kuwakamata watuhumiwa wanaodaiwa kushiriki mauaji hayo na kuelekeza eneo ulipotupwa mwili.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI