Header Ads Widget

KAMBI ZA MADAKTARI BINGWA ZAUNGWA MKONO KIGOMA


Na Fadhili Abdallah,Kigoma

WANANCHI wa mkoa Kigoma wamesema kuwa kambi za huduma za matibabu ya Kibingwa  zinazofanyika kwenye maeneo mbalimbali mkoani humo yamekuwa msaada mkubwa kwa kuwezesha kusogezwa karibu kwa huduma hizo sambamba na kupunguza gharama kwa wananchi wanaohudhuria kupata matibabu kwenye kambi hizo.

Hayo yameelezwa wakati wa kufungwa kwa kambi ya matibabu iliyokuwa ikisimamiwa na taasisi isiyo ya kiserikali ya  Empower Society, Building the Nation (ESBN) yaliyofanyika katika mji mdogo wa Uvinza mkoani Kigoma ambapo huduma hizo zilikuwa zikitolewa bila malipo.

Mmoja wa wananchi hao Robinson Bakayemba mkazi wa Uvinza mkoani Kigoma ambaye alihudhuria huduma za matibabu katika kambi hiyo alisema kuwa imewarahisishia na kuwasogozea huduma karibu lakini pia katika kambi hiyo hawakulipa gharama zozote za vipimo, ushauri wala dawa waliozokuwa wakipewa.


 Naye  Zuhura Chubwa mkazi wa kitongoji cha Kashakari mji mdogo wa Uvinza mkoani Kigoma alisema kuwa kwa muda mrefu alikuwa anasumbuliwa na tumbo lakini hakuwa na fedha na hospitali ya wilaya Uvinza kuna umbali Zaidi ya kilometa 20 hivyo ujio wa madaktari hao umewezesha kufanyiwa uchunguzi na kupata matibabu.

Akieleza kuhusu uwepo wa kambi hiyo ya madaktari Bingwa inayotembea Mratibu wa huduma hizo, Mbwana Mwinyi Mkuu ambaye ni Afisa utafiti kutoka taasisi ya ESBN alisema kuwa kambi hiyo ya Uvinza mkoani Kigoma ni ya pili kwa mwaka huu baada ya ile ya awali iliyofanyika wilaya ya Lushoto mkoani Tanga.

Mwinyimkuu alisema kuwa kambi hiyo imefanyika mkoani Kigoma kusaidia serikali katika kusogeza huduma kwa wananchi hasa mkoa huo uliompakani na nchi za ukanda wa maziwa makuu ambapo kwa siku nne waliyofanya kambi hiyo jumla ya watu 700 wamefika kwenye kambi hiyo na kupata huduma na damu chupa 44 zimekusanywa.

Akifunga kambi hiyo Mkuu wa wilaya Uvinza, Dinnah Mathamani alisema kuwa wanawashukuru wadau  kwa kuunga mkono serikali katika kufikisha huduma za matibabu karibu na wananchi na kwamba hiyo ni sehemu ya kusaidia serikali ambayo imefanya kazi kubwa katika kuboresha huduma za afya nchini.

 

Mathamani alisema kuwa serikali ndiyo msimamizi mkuu wa kambi hizo za matibabu zikiongozwa na kambi ya matibabu ya Raisi Samia ambayo imefika maeneo mbalimbali na kwamba serikali ya mkoa huo bado inaendelea kuwasiliana na wadau mbalimbali kuhakikisha kambi hizo za matibabu zinafanyika kwa wingi Zaidi.

 

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI