Header Ads Widget

AZAKI HOI USAID KUJIONDOA

 

Uamuzi wa Rais wa Marekani,Donald Trump, kusitisha shughuli za shirika la Maendeleo ya kimataifa la Marekani(USAID) kumesababisha kusimama miradi yenye thamani ya zaidi ya trilioni moja na kufungwa kwa ofisi kadhaa za asasi za kiraia huku mamia ya wafanyakazi wakikosa ajira.

Rais Trump mwezi Februari mwaka huu, alitangaza kusitisha asilimia 80 ya miradi ambayo imekuwa ikifadhiliwa na USAID katika nchi kadhaa duniani, kwa kile ambacho alieleza kupunguza matumizi ya serikali yake .

Akiwasilisha taarifa ya utafiti uliofanywa na Mtandao wa mashirika ya watetezi wa haki za binaadamu nchini(THRDC),kuhusiana na athari za USAID kujiondoa ghafla na uhimilivu wa asasi za kiraia nchini,katika maadhimisho ya wiki ya azaki 2025 jijini Arusha, Mratibu wa kitaifa wa THRDC Wakili Onesmo ole Ngurumwa alisema imebainika asilimia 50 ya Azaki nchini zilizokuwa zinapata fedha  kutoka USAID zimeathirika sana.


Ole Ngurumwa alisema katika utafiti huo ambao bado takwimu zinakusanywa, uliotokana na dodoso lililojazwa na azaki  nchini,imebainika kuwa miongoni mwa waathirika wakubwa ni  mashirika makubwa ya kimataifa , mashirika ya dini,mashirika yaliyokuwa na miradi ya  afya, uhifadhi na mazingira ,miradi ya maji, masuala ya haki za binaadamu na masuala ya ukuzaji demokrasi na utawala bora nchini.

" Kuna mashirika yamefunga ofisi, mengine yamepunguza wafanyakazi, mengine yanakabiliwa na ukata mkubwa na mwaka huu tuna uchaguzi mkuu USAID kupitia mashirika yake makubwa wamekuwa wakitoa ufadhili wa Azaki ili zitowe elimu ya mpiga kura na nyingine kuwa waangalizi wa uchaguzi  mwaka huu fedha zao hakuna hivyo ushiriki za azaki katika uchaguzi utapungua sana "alisema

 Alisema katika utafiti huo. imebainika kuwa mchango wa  sekta ya Azaki nchini kwa taifa unatarajiwa kupungua kwa zaidi ya asimilia 50, ambapo  takwimu zinaonesha mwaka uliopita mchango ulifikia zaidi ya trilioni mbili ambapo USAID ndio walikuwa wafadhili wakubwa wa miradi nchini.

" Kwa takwimu tulizonazo Kwa mwaka 2023 Tanzania ilipokea Dola milioni 630 (takriban Sh. Trilioni 1.61) na kuifanya kuwa miongoni mwa nchi 20 zilizoongoza kwa kupokea misaada kutoka USAID huku ikishika nafasi ya 10 duniani na ya 10 barani Afrika na tunatarajia kukutana na Ubalozi wa Marekani hapa nchini kupata takwimu zaidi"alisema.

Alisema kilichotokea kutokana na USAID kusitisha ufadhili ni fundisho kubwa kwa Azaki na sasa zinapaswa kuanza kutafakari na kuwa na mikakati mipya ya kuwa na uhimilivu  katika mapato na kutafuta mbinu mpya za kujipatia ufadhili wa miradi badala ya kutegemea kutoka nje ya nchi pekee.

" Tunaendelea na majadiliano katika maadhimisho haya kuona jinsi gani Azaki zinaweza kuhimili hali ya sasa ya kupungua kwa ufadhili kutoka mashirika makubwa ya kimataifa na kujengeana uwezo wa mbinu mbadala"alisema

Ole Ngurumwa alisema kujiondoa kwa USAID sio tu kumeathiri Azaki nchini bali pia hata uchumi wa taifa kwani sasa kumechangia kupungua kwa mzunguko wa dola za Marekani nchini kutokana na  kusitishwa kwa ufadhili wa miradi mingi .

"Takribani dola milioni 500 zilizokuwa zimetengwa kwa miradi ya mashirika ya kiraia, makampuni, na miradi mingine ya maendeleo mwaka 2024 zitabaki zimeganda hadi kutakapopatikana maelekezo mapya kutoka kwa serikali ya Trump"alisema


Katika maadhimisho hayo, pia Wana azaki walijadiliana juu ya mwenendo wa mashirika mengine makubwa ya kimataifa, kuanza kupewa fedha za kuendesha miradi yao moja kwa moja nchini, badala ya kupitia kwenye asasi ndogo za ndani ya nchi ama kuwa na ubia.

Akichangia mjadala huo, Ole Ngurumwa alisema azaki hazipingi mashirika makubwa ya kimataifa kutekeleza miradi yao moja kwa moja nchini lakini inashauri yashirikiane na mashirika ya ndani , ili pia kuyajengea uwezo wa kufanyakazi kwa viwango vya kimataifa.






Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI