Header Ads Widget

DC KIGOMA AIPONGEZA MAIN FM KUIBUA VIPAJI VYA MICHEZO .


Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Dkt Rashid Chuachua akiongea na waandishi wa habari (hawapo pichani) kwenye hafla ya uchezeshwaji wa droo ya timu za mpira ambazo zitashiriki katika mashindano ya mpira wa miguu ya Main FM Cup kwa msimu wa pili.


Na Editha Karlo, Kigoma.


MKUU wa Wilaya ya Kigoma mjini Dkt. Rashid Chuachua ameupongeza uongozi mzima wa kituo cha redio cha Main FM kwa jinsi kinavyoendelea kuonyesha kuwasaidia vijana kwa kuibua vipaji vyao vya michezo kwa kuandaa matukio ya kijamii ikiwemo mashindano ya mpira wa miguu.


Dkt Chuachua ameyasema  hayo kwenye ukumbi wa Kigoma social hall  katika hafla ya uchezeshwaji wa droo ya timu za mpira ambazo zitashiriki katika mashindano ya mpira wa miguu ya Main FM Cup kwa msimu wa pili.


Mkuu huyo wa Wilaya amesema kituo cha radio cha Main FM kimekuwa mstari wa mbele kuiunganisha jamii kupitia matukio mbalimbali ikiwa ni pamoja na uendelezaji wa Ligi Main FM Cup inayoenda kufanyika kwa msimu wa pili.


"Kwakweli ninatoa pongezi zangu za dhati kwa uongozi wa Radio ya Main FM mbali ya kuwa na kazi kuhabarisha umma kupitia radio yenu na kutangaza lakini mmekuwa na kazi ya zingine za kugusa maisha ya jamii ya wanakigoma kwa kutumia fursa nyingine kama hivi michezo nawapongeza kwa hili kwani mnagusa wanachi moja kwa moja"amesema Dkt Chuachua


Amesema kuwa uwekezaji unaofanywa na wadau mbalimbali katika sekta ya michezo unaleta mapinduzi makubwa kwenye sekta hiyo ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt Samia Suluhu Hassan anapenda kuona sekta ya michezo ikiwa katika taswira ya mapinduzi makubwa.


Naye Mkurugenzi wa kituo cha Radio ya Main FM Pascal William amesema lengo la kuanzishwa kwa mashindano hayo ni  sababu ya kutambua na kuthamini jitihada za madereva wa bodaboda(maofisa usafirishaji)katika Taifa.


"Pamoja na kupata burudani michezo kutoka kwenye timu hizo za bodaboda lakini lengo la mashindano hayo pia ni kuwakutanisha vijana rika mbalimbali  kuwaweka pamoja,kuibua vipaji,sambamba na kutoa elimu ya usalama barabarani na kukuza fursa za uchumi kwa vijana"amesema Mkurugenzi wa Main FM 


Pascal amesema michuano ya Main FM Cup 2025 itaanza kutimua vumbi tarehe 16 Mei na kuisha mwezi August 2025,katika viwanja vya Kawawa eneo la Ujiji kwa vijana wa bodaboda na Bajaji kuonyesha vipaji vyao.


MWISHO.


Mkurugenzi wa kituo cha radio cha Main FM Pascal William akiongea kuhusu msimu wa pili wa mashindano ya Main Fm Cup katika ukumbi wa kigoma social hall.


Mkuu wa Wilaya Kigoma Dkt Rashid Chuachua(wakatikati)azindua jezi kwaajili ya Main FM cup msimu wa pili 2025.


Baadhi ya viongozi na wawakilishi wa timu shiriki za Michuano Ya Main Fm Cup pamoja na wadau wengine wa michezo wa Mkoa wa Kigoma wa kifuatilia uchezeshwaji wa droo ya Main FM Cup 2025 iliyochezeshwa katika ukumbi wa kigoma social hall.


Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI