Na. Anangisye Mwateba-Bungeni Dodoma
Wizara ya Maliasili na utalii imetoa rai kwa wadau wa sekta ya utalii kuchangamkia fursa ya uwekezaji kwenye shughuli na huduma za utalii katika maeneo ya wilaya ya Kilwa kwenye Mapango ya Nang’oma, Namahengo, Likolongomba na Nampombo. Lengo ni kuhakikisha sekta ya utalii inaendelea kuchangia kwa kiasi kikubwa katika uchumi wa wananchi wa Kilwa na Taifa kwa ujumla.
Rai hiyo imetolewa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Dunstan Kitandula(Mb) wakati akijibu swali la Mhe. Francis Kumba Ndulane ambaye alitaka kujua Serikali ina mkakati gani wa kuvifanya vivutio vya Mapango ya Nang’oma, Namahengo, Likolongomba na Nampombo kuwa na tija kwa Taifa.
Aidha, Mhe. Kitandula aliongeza kuwa Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa imeanza kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuhakikisha vivutio vya mapango ya Nang’oma, Namahengo, Likolongomba na Nampombo vinakuwa na tija katika kuchangia kwenye pato la taifa.
Naibu Waziri alisema kuwa Mikakati hiyo ni pamoja na kuanzisha Adhimisho la Kumbukizi ya Vita ya Majimaji ambalo hufanyika Mwezi Agosti kila mwaka katika Wilaya ya Kilwa kwa lengo la kutangaza vivutio mbalimbali vya kilwa ikiwemo mapango hayo kwa wadau wa utalii, washiriki, waandishi wa habari na wananchi wanaotembelea katika tukio hilo.
0 Comments