Na Farida Mangube
Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA Kwa kushirikiana na shirika la misaada la watu wa Japan “Japan International Cooperation Agency” (JICA) wamekubariana kushirikiana kuibua ujuzi katika sekta ya kilimo na umwagiliaji kwa kupitia wataalam mbalimbali kwenda kwa wanafunzi chuoni hapa.
Akizungumza mara baada ya kupokea ujumbe wa wageni kutoka JICA ulioongozwa na Mwakilishi Mkuu wa JICA Tanzania Ndg. ARA Hitoshi, Profesa Samuel Kabote kwa niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma amesema kuwa lengo kubwa ni Japan kutoa uzoefu wao kwenye mambo mbalimbali ya kimaendeleo ikiwemo kilimo na umwagiliaji kwa kupitia wataalam mbalimbali wa Japan na Tanzania.
Prof Kabote amefafanua kuwa kati ya vitu vinavyovutia ni historia ya Japan ya kutokutawaliwa na nchi za kikoloni na hadi sasa imepiga hatua kubwa katika maendeleo hususani katika sekta ya kilimo, hivyo ujuzi huo utatumika kwa wanafunzi wa Tanzania ambapo SUA na JICA wameandaa mkutano maalum utakao jumuisha wanafunzi na wataalam hao kwa kuwa wanafunzi wa chuo ni taifa la kesho. Hivyo mkutano huo mbali ya kushirikishana ujuzi utaelezea hatua mbalimbali ambazo nchi ya Japan ilifanya na kuweza kufika hapo ilipo katika maendeleo hasa kilimo.
Kwa upande wake Afisa Mradi wa JICA CHAIR Ndugu Alfred Zakaria amebainisha kuwa ujio wao wa sasa ni maandalizi ya kikao kikubwa kinachotarajiwa kufanyika chuoni hapa kwa lengo la kubadilishana ujuzi. Hivyo amewaalika wanafunzi wote wajitokeze katika mkutano huo ili waweze kupata ujuzi kutoka kwa maprofesa mbalimbali wa Tanzania na Japan.
0 Comments