Header Ads Widget

WAFANYABIASHARA MOROGORO WAIPA KONGOLE TRA

 


Maafisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA),Mkoa wa Morogoro,wakiwapatia huduma ya ulipaji wa kodi baadhi ya Wafanyabiashara katika Manispaa ya Morogoro,baada ya kuweka kambi katika eneo la Soko Kuu la Chifu Kingalu lilopo Manispaa ya Morogoro, picha na Ashton Balaigwa.



Na Ashton Balaigwa,MOROGORO

WAFANYABIASHARA Mkoani Morogoro wameonyeshwa kuridhishwa na hatua ya  Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA),kwa kuweka kambi katika maeneo mbalimbali ili kuwapatia huduma za ulipaji kodi kwa wakati  na kuwaepusha kulipa faini baada ya muda wa ulipaji  uliwekwa kufikia tamati.


Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa utoaji wa huduma za mlipakodi  katika  Soko Kuu la Chifu Kingalu , Manispaa ya Morogoro  , wafanyabishara hao walisema,kuwekwa kwa kambi hizo inachangia huduma   kuharakisha kwao ulipaji kodi kwa wakati na kuepukana na kutozwa riba .


Mfanyabiashara Shabani Kibuhile alisema kwa sasa Mamlaka hiyo imekuwa na desturi ya kutoa huduma rafiki kwa jamii tofauti na miaka iliyopita ambapo njia waliyokuwa wakiitumia iliwafanya wafanyabishara kuwakimbia  na kuwaona ni maadui.


Kibuhile alisema kuwa , wananchi wakiwemo wafanyabiashara wanapolipa kodi kwa wakati wanachangia  upatikanaji wa huduma bora kwa Watanzania zikiwemo za miundombinu ya barabara ,huduma za afya ,elimu na nyingine mtambuka.


“ Hivi sasa TRA  huduma zao zimekuwa  rafiki  kwa sisi wafanyabiashara kwani wanatoa elimu, kushauri, kuelekeza masuala  ya msingi  na umuhimu wa kulipa  kodi yenyewe ndiyo maana wamekuwa wakitufuata tulipo  tofauti na miaka ya nyuma ilikuwa ni kukimbizana “alisema Kibuhile.


Mfanyabiashara huyo aliwashauri wananachi na  wenzake kujenga utaratibu wa kufuata sheria ulipaji kodi  wakitambua Mamlaka hiyo ina  jukumu la kusimamia sheria za kodi  ili  kuiendeleza nchi yetu ,na nchi haiwezi kuendelea bila kulipa kodi .


Naye mfanyabiashara , Ijumbo Majani  ,alisema  kusongezwa kwa huduma za Mamlaka hiyo  karibu yao  imewarahisishia kuipata huduma za mlipakodi  bila ya kukabiliana na changamoto ikiwa ya kuwafuata ofisini kwao.


“ Nimekuja hapa  kwenye kituo cha Soko Kuu la Chifu Kingalu na nimetumia dakika chache kuhudumiwa huduma ya malipo serikalini  na ninarudi kuendelea na biashara zangu “ alisema  Majani.


Majani alishauri  huduma iwe ni endelevu kwa kuwa  itawawezesha wananchi na wafanyabiashara kulipa kodi kwa muda unaopangwa licha ya wao  kutambua ni wajibu wao  kulipa kodi ya serikali.


Kwa upande wake  Ofisa Huduma na Elimu ya Mlipakodi wa TRA mkoa wa Morogoro, Immaculate Chaggu alisema,  huo ni   mwendelezo wa kukusanya mapato kwa kutoa namba ya malipo ya serikali kwa wafanyabiashara na utoaji  elimu ya mlipa kodi.


 “ Tumeweka Kambi katika maeneo matatu ikiwemo  eneo la Soko Kuu la Chifu Kingalu ili tuwahamasishe walipa kodi waweze kulipa kodi yao kwa awamu ya tatu bila shuruti ili wasiweze kupata riba baada ya muda kupita “ alisema Chaggu .


Alisema huduma zimesongezwa karibu na wananchi  kwa kuweka  vituo vitatu  ambavyo ni Soko Kuu la Chifu Kingalu , Kihonda na Mkundi  katika  Manispaa ya Morogoro.


Chaggu alisema vituo hivyo vilianza kutoa huduma Septemba 21, mwaka huu na  zaidi ya wateja 100 wanahudumiwa kwa  siku na kadri zinavyo karibia  mwisho wa kufikia  Septemba 30, mwaka huu idadi  inaendelea kuongezeka kwa siku.


Ofisa Mwandamizi wa Kodi wa Mamlaka hiyo mkoani Morogoro, George Mkope ,alisema  kupitia utekelezaji wa huduma hiyo kumekuwa na mwamko mkubwa wa wananchi kulipa kodi kwa hiari na njia hiyo  imeongeza morali kwao kujitokeza kulipa kodi kwa hiari .

“ Tunakusudia  kuongea vituo zaidi ili tuwafikie  watu wengi walipe  kodi kwa wakati na tufikie yale malengo tuliyopewa na serikali ya kukusanya  kodi “ alisema  Mkope.




Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI