Karibu Kwenye kitabu cha Laws of Human Nature, kilichoandikwa na Robert Green ikumbukwe kuwa Green ametupa sheria 18 za kuijua asili ya binadamu, akitupa mifano halisi iliyowahi kutokea kwa watu waliozingatia sheria hizi na wakafanikiwa au walizipuuza na kushindwa.
Laws of Human Nature ni kitabu ambacho kila mtu anapaswa kukisoma kwa sababu kimeeleza asili yetu binadamu tulivyo bila ya kuficha chochote. Tunaziona zetu halisi na hata za wengine, tunajifunza udhaifu mkubwa uliopo ndani yetu ambao unatufanya kushindwa kwenye mengi na pia tunajifunza jinsi ya kuvuka udhaifu tulionao ili tuweze kuwa na maisha bora na ya mafanikio.
Karibu kwenye tano za juma, tujifunze asili yetu, tujijue vizuri ili tuweze kuishi kwa ukamilifu na kutumia uwezo mkubwa uliopo ndani yetu kufanya makubwa zaidi.
#1 NENO LA JUMA; IJUE ASILI YA BINADAMU.
Asili ya binadamu ni kitu ambacho kila mmoja wetu angepaswa kuwa anakijua, kwa sababu ni kitu kinachotuhusu sisi wenyewe. Lakini jambo la kushangaza ni kwamba, hili ni eneo ambalo hatuna uelewa kabisa. Kwa kifupi hatujijui sisi wenyewe na wala hatuwajui wengine. Tunaishi maisha yetu kama watalii ambao wamejikuta kwenye miili yetu na tunaendeshwa tu na hisia bila ya kukaa chini na kufikiri kwa kina haya maisha yanatupeleka au tunayapeleka wapi.
Kitu kimoja ambacho kinatuzuia tusiijue asili yetu ni ubishi wetu, hatutaki kukubali kwamba hatujijui. Mfano najua unaposoma hapa unakataa kwamba wewe siyo mmoja wa wasiojijua, kwamba wewe unajijua vizuri.
Kama ndivyo nikuulize swali moja, je umewahi kuweka malengo na mipango mizuri, labda unajiambia kesho utaamka mapema na kutekeleza majukumu yako. Hiyo kesho muda wa kuamka unafika, lakini huamki, hata unapoamka unashindwa kutekeleza yale uliyopanga? Je unafikiri nini kinakwenda kinyume na malengo na mipango yako? Kama hujui basi huijui asili yako.
Kitu kingine; je umewahi kujiambia hutafanya kitu fulani, labda kumsema mtu vibaya, au kujihusisha na mahusiano fulani, au kudanganya. Lakini unakuja kujikuta umefanya, unapojiuliza unasema shetani alikupitia? Kama ndiyo basi jua huijui asili yako.
Cha mwisho muhimu zaidi; umewahi kumwamini mtu fulani, labda ni mwenza wako, au mtu unayefanya naye biashara, au kiongozi fulani, kwa nje anaonekana ni mwaminifu kabisa na unaweza kumtetea kwamba hawezi kufanya kitu cha ajabu. Lakini siku unakuta amefanya kitu ambacho hukutegemea afanye, unashtuka kwamba hukutegemea afanye hivyo. Kama umewahi kukutana na hali kama hii, basi huijui kabisa asili ya binadamu. Maana kama ungekuwa unaijua, ungeona dalili za yeye kufanya hivyo mapema kabla hajafanya. Kwa sababu kwanza, watu huwa hawafanyi kitu mara moja pekee, na pili watu wanaweza kuficha siri kwenye maneno, lakini matendo na lugha ya mwili inaeleza wazi kabisa.
Rafiki, kwa jinsi tunavyoona makosa tunayoyafanya kila siku kwenye maisha yetu, kuanzia kwetu wenyewe na hata kwa wale wa karibu yetu, suluhisho ni moja, tunapaswa kujifunza na kujua asili ya binadamu. Kwa sababu ni uelewa huo pekee utakaotuwezesha kujijua wenyewe, kujua uimara na udhaifu wetu na kupiga hatua. Pia tutaweza kuwajua wengine vizuri, kuelewa uimara na udhaifu wao, kuwajua mapema watu ambao ni matatizo na hata kuona vitu ambavyo watu wanaficha tusione.
Mwandishi Baltasar Gracian amewahi kunukuliwa akisema, watu wanatumia muda mwingi kujifunza tabia za wanyama na mimea, badala ya kutumia muda huo kujifunza tabia za binadamu ambao wanaishi nao kila siku! Kama anavyotuambia Baltasar, tukiweka nguvu zetu katika kujifunza tabia za watu, tutaweza kuwa na maisha bora na mahusiano mazuri na wengine.
Kwenye kitabu chake cha 48 Laws Of Power, Robert Green anasema, mahusiano ya binadamu yanahusisha kusema uongo na kudanganya, anasema kitu pekee kinachotutofautisha sisi binadamu na wanyama wengine ni uwezo wetu wa kusema uongo na kudanganya kwa vitendo.
Kama hivi ndivyo watu walivyo, unaweza kuona ni jinsi gani kutokuijua asili ya binadamu kunavyokugharimu. Hivyo amua leo kwamba utaweka kipaumbele kwenye kujifunza asili na tabia za binadamu, ili ujijue vizuri wewe mwenyewe na uwajue wengine pia.
Na sehemu sahihi ya kuanzia elimu yako ya kuijua asili ya binadamu ni kwenye kitabu hiki cha The Laws of Human Nature.
#2 KITABU CHA JUMA; SHERIA 18 ZA ASILI YA BINADAMU.
Rafiki yangu mpendwa,
Kama nilivyokueleza hapo juu, juma hili tunakwenda kujifunza kwa kina kutoka kitabu kinachoitwa The Laws of Human Nature ambacho kimeandikwa na Robert Greene. Kitabu hiki kimeshiba kweli kweli, kimechambua kwa kina sana sheria 18 za asili ya binadamu, na kwenye kila sheria kuna mfano wa watu waliotumia au kupuuza sheria hiyo na matokeo waliyopata.
Katika uchambuzi huu, nakwenda kukushirikisha sheria hizi 18 za asili ya binadamu na hatua za kuchukua kwenye kila sheria ili uweze kuwa na maisha bora.
SHERIA YA KWANZA; KUTOKUFIKIRI.
Huwa tunadhani ya kwamba tunadhibiti mwenendo wa maisha yetu, kwa kupanga na kufikiri kila hatua tunayopiga kwenye maisha. Lakini ukweli ni kwamba, hatufanyi maamuzi yetu kwa kufikiri, badala yake tunafanya kwa hisia.
Kwa sehemu kubwa tunaendeshwa na hisia na siyo kufikiri. Tunaweza kujidanganya kwamba tunafikiri, lakini huwa tunafanya maamuzi kwa hisia kwanza kisha baadaye tunayahalalisha kwa kufikiri.
Tunapaswa kuondokana na hali hii ya kuongozwa na hisia na kuanza kufikiri kwa kina kwenye kila maamuzi unayofanya. Tunapaswa kujilazimisha kuona vitu na hali kama zilivyo na siyo kwa jinsi tunavyotaka kuona.
Hili siyo jambo ambalo linakuja kirahisi kwetu sisi binadamu, bali ni jambo ambalo tunapaswa kujifunza na kufanyia kazi. Inawezekana kama tutajipa muda katika kufikiri, kuepuka kufanya maamuzi ya haraka na kuacha kuangalia wengine wanafanya nini.
SHARIA YA PILI; MAJIVUNO.
Huwa tuna tabia ya kujivuna, kujiona sisi ni bora kuliko watu wengine. Hali hii ya majivuno inatofautiana baina ya watu, kuna ambao wanajiona wao ndiyo wa muhimu zaidi kuliko wengine. Tunataka dunia nzima ituzunguke sisi, kila mtu atusikilize sisi na hata tunapokuwa kwenye mazungumzo na watu wengine, tunajisifia zaidi sisi kuliko wengine.
Kwa vyovyote vile, majivuno siyo mazuri kwenye maisha, kujiona sisi ni wa maana na muhimu kuliko wengine kunaharibu mahusiano yetu na watu wengine.
Njia pekee ya kuondokana na majivuno ni kuwa na utu na uelewa kuhusu wengine. Kujua na kuonesha kila mtu ni muhimu na kujali hali na hata maoni ya wengine. Kuacha kujiongelea wewe mwenyewe na kuwapa watu nafasi ya kujiongelea wao pia.
Pia epuka sana wale watu ambao wamezama kwenye majivuno kiasi kwamba hawajali kabisa kuhusu wengine. Hawa ni watu ambao wameshapotea na hawawezi kurudi tena kwenye uhalisia, kuhangaika nao utaishia kuumia mwenyewe.
SHERIA YA TATU; BARAKOA.
Binadamu tuna tabia ya kuvaa barakoa (masks) ambazo zinatuonesha kuwa watu wazuri na wanaojali. Kwa nje tunaonekana ni wastaarabu, waaminifu, na tunaojiamini. Lakini ndani mambo ni tofauti kabisa. Hivi ndivyo binadamu tunavyodanganyana kila siku, hivyo kama utafanya maamuzi kuhusu mtu kwa mwonekano wa nje, jua utaishia kufanya makosa makubwa kwenye maisha yako. Kile unachoona nje, siyo uhalisia wa mtu, bali sanamu ambayo mtu ameitengeneza uione.
Jifunze kuona nyuma ya sanamu ambazo watu wamevaa, jifunze kuangalia zaidi ya mwonekano wa nje. Kwenye kila sanamu ambayo mtu amevaa, kuna ufa ambao unaonesha uhalisia wa mtu huyo. Watu huwa wanaonesha matendo na hisia zao kwa njia ambayo siyo ya moja kwa moja. Kama utakuwa makini utaweza kuona kile ambacho watu wanaficha.
Kwa upande wa pili, kwa kuwa watu wanakuhukumu kwa mwonekano wako wa nje, basi unapaswa kujijengea mwonekano ambao ni bora. Jijengee mwonekano ambao utaleta kuheshimika na kuaminika kwa wale unaotaka wafanye hivyo. Lakini usifanye hivyo kwa kudanganya tu, bali fanya ikusaidie katika kuboresha mahusiano na ushirikiano na wengine.
SHERIA YA NNE; TABIA.
Unapochagua mtu wa kushirikiana naye kwenye jambo lolote, ni rahisi sana kushawishika na maneno na mwonekano wa mtu. Lakini vitu hivyo ni rahisi kukudanganya na kukupoteza. Watu wanaweza kuahidi na kujisifia watakavyo, wanaweza kutengeneza mwonekano mzuri wa nje na ukakushawishi sana.
Kuujua ukweli kuhusu watu ili uweze kufanya maamuzi ya kushirikiana nao, angalia tabia za watu, hasa tabia za nyuma. Angalia mwenendo wao wa maisha, mambo ambayo wamewahi kukamilisha na waliyowahi kushindwa. Angalia kipindi ambacho wamekutana na magumu, waliwezaje kuyavuka. Angalia mahusiano yao ya nyuma na watu wengine.
Tabia za mtu za nyuma zinamweleza yeye kwa ukweli kuliko sifa anazokuambua kwa mdomo. Hili ni muhimu sana kuzingatia pale unapochagua mtu wa kumwajiri au kuajiriwa naye, pia unapochagua mtu wa kufanya naye biashara. Mfano kama mtu anakuambia ni mchapa kazi, lakini ukiangalia kwenye historia yake ya nyuma alishafukuzwa kazi maeneo matatu tofauti, haijalishi atakupa sababu gani, ana tatizo.
Tabia za watu huwa zinajirudia, na huwa zimejichimbia ndani kabisa kwenye mfumo wao wa maisha, hivyo kabla hujafanya maamuzi kuhusu mtu, angalia kwanza tabia zake, kwa yale yanayoonekana na siyo anayokuambia.
wengine pia.
#PATA KITABU NA UCHAMBUZI ZAIDI.
Rafiki yangu mpenda, kama ungependa kupata kitabu tulichochambua kwenye makala hii ya tano za juma, pamoja na kupata uchambuzi wa mafunzo zaidi kutoka kwenye kitabu hiki, karibu ujiunge na channel ya TANO ZA MAJUMA 52 YA MWAKA.
Hii ni channel ambayo ipo kwenye mtandao wa TELEGRAM MESSENGER, ambapo kila juma nakutumia kitabu cha juma, uchambuzi huu na mafunzo ya ziada yote kwa mfumo wa pdf ambapo utaweza kusoma na hata kuhifadhi vizuri kwa matumizi ya baadaye. Pia kwa kujiunga na channel hii, utaweza kupata mafunzo yote ya nyuma na hata ukipoteza mafunzo hayo utaweza kuyapakua tena muda wowote unapoyataka. Chanzo :Mitandao ya kijamii
KARIBU KUJIUNGA NA MATUKIO DAIMA APP KWA HABARI ZAIDI
0 Comments