Na Fadhili Abdallah,Kigoma
Wahudumu wa Afya ngazi ya Jamii mkoani Kigoma wamepewa msaada wa baiskeli 250 ili ziwasaidie kutekeleza majukumu yao kwa urahisi na ufajisi katuka kuifikia jamii ili iweze kupata huduma za matibabu katika kutekeleza mpango wa serikali wa afya kwa wote ikiwemo kukabili vifo vya mama wajawazito na Watoto wakati wa kujifungua.
Msaada huo wa baiskeli ni ufadhili kutoka Shirika lisilo la kiserikali la Catholic Relief Services (CRS) kwa ajili ya kurahisisha ufuatiliaji na utoaji huduma za afya kwa jamii hasa kusaidia kupunguza vifo vya wajawazito na watoto wakati wa kujifungua katika maeneo ya vijijini
Akizungumza katika hafla ya kukibidhi baiskeli hizo Mkuu wa mkoa Kigoma, Thobias Andengenye amewataka wahudumu wa afya ngazi ya jamii walionufaika na vitendea kazi hivyo kuvitumia kuendana na miongozo ya matumizi iliyowekwa na serikali.
Andengenye alisema kuwa Serikali ya Awamu ya Sita kupitia Wizara ya Afya imedhamiria kushirikiana na wadau wa Afya ili kuboresha Afya, Lishe na Ustawi wa wakazi mkoani Kigoma na Tanzania kwa ujumla sambamba na mkazo katika kudhibiti vifo ya mama wajawazito na watoto wakati wa kujifungua.
Kwa upande wao wahudumu wa afya ngazi ya jamii akiwemo Esther John ameishukuru Serikali ya awamu ya sita kupitia uongozi wa serikali Mkoa wa Kigoma kwa kuendelea kushirikiana na wadau wa Maendeleo katika Sekta ya Afya ambapo alisema kuwa nyenzo hizo za usafiri itakuwa chachu katika utendaji kazi wao ikiwemo kuwafikia wananchi kwa wakati.
Akizungumza katika makabidhiano hayo Mganga Mkuu wa mkoa Kigoma,Damas Kayera alisema kuwa kutolewa kwa msaada huo kwa wahudumu wa afya ngazi ya jamii kutakuwa msaada mkubwa kwao idara ya afya ngazi ya mkoa kupata taarifa mbalimbali za wagonjwa waliopo majumbani na kuwezesha kuchukua hatua kwa haraka sambamba na ukusanyaji wa takwimu ya masuala ya afya.
Mwisho
0 Comments