Na Gabriel Kilamlya Matukio DaimaAPP NJOMBE
Wananchi wa kijiji cha Ujindile Kata ya Igosi Wilaya ya Wanging'ombe mkoani Njombe wameondokana na changamoto za migogoro ya ardhi ambayo imekuwa ikisababisha vurugu baada ya serikali kupima ardhi kwa wakazi 675.
Katika zoezi la uzinduzi wa ugawaji Hatimiliki za kimila kwa wananchi hao Mkurugenzi wa shirika la urasimishaji ardhi la Land Tenya Assistance (LTA) Malaki Msigwa amesema kupimwa kwa maeneo hayo kunawasaidia wananchi kuwa na uhalali kisheria wa kumiliki ardhi yao.
Akikabidhi hati hizo mkuu wa wilaya ya Wanging'ombe Claudia Kitta amewataka wananchi wote kuhakikisha wanapima ardhi yao kwa kuwa inasaidia sana kuondoa changamoto ya migogoro ambayo imekuwa ikisababisha hadi mauaji.
Awali Diwani wa kata ya Igosi Damascus Mgaya na wananchi wa Ujindile wamesema kupatikana kwa hati hizo kutawafanya waishi kwa amani kwa kuwa kila mmoja eneo lake sasa linatambulika kisheria.
Naye Ofisa ardhi halmashauri ya wilaya ya Wanging'ombe Bwana Nail Mbopyo na Godfrey Masunga Kaimu Kamishna msaidizi wa ardhi mkoa wa Njombe wamewataka wananchi Kuzitunza hati hizo kwa kuwa zikiharibika Zitashindwa kuwasaidia.
Urasimishaji wa ardhi utakwenda kuwa muarobaini wa migogoro yote inayotokana na ugomvi wa mashamba na viwanja ambayo imekuwa changamoto kubwa katika maeneo mengi hapa nchini.
0 Comments