Na Gift Mongi MATUKIO DAIMA APP
DAR ES SALAAM
Tume ya ushindani nchini(FCC)imeombwa kuingilia kati bidhaa za ngozi(bandia)zinazoingizwa kutoka nje ya nchi zenye mfanano na zile zinazozalishwa hapa nchini.
Kuingia kwa bidhaa hizo kunatajwa kuwa ni kichocheo kimojawapo katika kuua viwanda vya ndani jambo ambalo linaweza kuathiri uchumi moja kwa moja.
Kenneth Woisso ni mkurugenzi wa kiwanda cha bidhaa za ngozi(WOP)Woisso Original Product ambapo alisema kuendelea kuingia kwa bidhaa hizo ni tatizo ambalo linatakiwa kuchukuliwa kwa hatua za kipekee.
'Soko la bidhaa kutoka China ni kubwa na mbaya zaidi bidhaa zao ambazo sio ngozi halisi zinauzwa kwa bei ya chini hivyo sisi wazalishaji wa ndani tunapitia wakati mgumu'alisema Woisso
Katika hatua nyingine mkurugenzi huyo wa WOP aliiomba serikali kuona namna ya kuongeza tozo kwa bidhaa za ngozi zinazotoka nje ili kuwezesha kukua kwa viwanda vya ndani vya bidhaa hizo.
Alisema kuongeza tozo hiyo licha ya kupunguza uingizwaji wa bidhaa hizo kutaenda kuimarisha soko la ndani lakini pia kukua kwa mazao ya ngozi nchini
'Tozo ikiwekwa nadhani wale wenye kuingiza hizi bidhaa watapungua hivyo viwanda vya ndani vitaenda kuongeza uzalishaji lakini mazao ya ngozi kwa ujumla yataenda kufanya vizuri'alisema
Gerald Hiza ambaye ni mzalishaji mdogo wa bidhaa za ngozi alisema biashara hiyo kwa sasa inapitia wakati mgumu kutokana na soko kuingiliwa na bidhaa ambazo si halisi(bandia)za ngozi na kutaka jitihada za maksudi kufanyika ili kuokoa soko la ndani
'Wenzetu China wana akili nyingi katika soko la hizi bidhaa utakuta zao ni nyingi na usipokuwa makini utadhani ni ngozi kumbe sio ni bandia sasa ifanyike hatua za maksudi ili tuponye viwanda vyetu'alisema
0 Comments