Na Hamida Ramadhan Matukio Daima app Dodoma
IBADA maalum ya kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Edward Sokoine inatarajiwa kufanyika Ijumaa April 12,mwaka huu ambapo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kushiriki.
Hayati Sokoine alikuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika vipindi viwili wakati wa uongozi wa Awamu ya Kwanza ambapo alizaliwa Agosti 01, 1934, kijijini Enguik, Monduli Juu wilayani Monduli, mkoani Arusha.
Akizungumza na Waandishi wa Habari leo Alhamisi Marchi 28 Jijini Dodoma Msemaji wa familia ya Hayati Sokoine,Lembris Kipuyo amesema ibada hiyo itafanyika katika Kijiji Cha Enguik Monduli Juu Wilayani Monduli Mkoani Arusha.
"Nawaalika watanzania wote kwenye ibada maalum ya kumbukizi ya miaka 40 ya Hayati Edward Moringe Sokoine, aliyekuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, itakayofanyika Ijumaa Aprili 12, 2024, katika Kijiji cha Enguik, Monduli Juu mkoani Arusha.
"Ibada hiyo itakayofanyika siku ya Ijumaa Aprili 12, 2024, saa 3:00 asubuhi, imeandaliwa na familia ikishirikiana na Taasisi ya Hayati Edward Moringe Sokoine.
Amesema ibada hiyo ya kumbukumbu ya Hayati Sokoine itawashirikisha viongozi mbalimbali wa Serikali wakiongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Amesema lengo kubwa la kuanzishwa kwa Taasisi ya Hayati Edward Moringe Sokoine, ni kuenzi mema aliyoyafanya, kwani aliacha alama kubwa ambayo taifa linamkumbuka hadi leo.
"Taasisi hiyo imejikita katika masuala ya elimu, kilimo, hifadhi ya mazingira, vyanzo vya maji pamoja na afya.
Amesema hayati Sokoine alikuwa mzalendo wa kweli, alipenda taifa lake na wananchi wake, alihakikisha kwamba rasilimali za nchi zinatumika na watanzania wote, aliwatumikia wananchi bila kubagua na alikuwa na hofu ya Mungu katika kufanya kazi zake.
0 Comments