NA MWANDISHI WETU, MATUKIO DAIMA App DAR
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka wathamini wote wawe waadilifu, wenye weledi na wazingatie miiko ya taaluma katika kazi zao za kila siku.
Majaliwa amesema kuwa wathamini ni watu muhimu katika kufanikisha mipango ya maendeleo ya Taifa.
“Mnapaswa kuwa waadilifu na kuzingatia thamani halisi ya ardhi, jengo au chochote kinachofanyiwa uthamini,” amesema.
Amesema hayo wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Nne wa Mwaka wa Wathamini unaofanyika kwa siku mbili katika Kituo cha Mikutano cha Jakaya Kikwete, jijini Dodoma.
“Kazi ya uthamini si ya wababaishaji au vishoka, hivyo basi kila mthamini hana budi kuthamini na kuheshimu taaluma yake.”
Majaliwa amesisitiza kuwa: “Wapo baadhi ya wathamini ambao si waadilifu kwa kushirikiana na watendaji wengine hutoa makadirio ambayo hayawiani na thamani halisi. Vitendo hivyo husababisha kupoteza mapato ya Serikali lakini pia kuwanyima haki wale wanaostahili kupata haki.”
Aidha, Majaliwa amewataka watendaji wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi hususani wathamini washirikiane na sekta binafsi kufanya kazi za uthamini.
“Tumieni fursa ya uwepo wa wathamini binafsi ili kutoa huduma bora na ya haraka hapa nchini, kufanya hivyo mtakuwa mnatekeleza maagizo ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya ushirikishaji wa sekta binafsi kwa maendeleo ya Taifa.”
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu Majaliwa amewataka wathamini hao watumie mkutano huo kufanya majadiliano ya kina kuhusu masuala ya taratibu za utwaaji ardhi na sheria zake, ukokotozi wa fidia katika maeneo ya madini, viwango vya thamani ya ardhi na mazao, changamoto za kisera za utwaaji ardhi pamoja na kupata suluhu ya malalamiko ya wananchi.
0 Comments