Header Ads Widget

ZITTO KABWE AITAKA SERIKALI KUHARAKISHA MCHAKATO JUU YA KATIBA MPYA

Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Kiongozi wa Chama cha ACT Wazalendo Taifa Mhe. Zitto Kabwe leo amehutubia Mkutano wa hadhara katika Mkoa wa Shinyanga  huku akiitaka serikali kuharakisha mchakato wa marekebisho ya sheria ya mabadiliko ya katiba.

Mkutano huo wa hadhara umefanyika kwenye uwanja wa zimamoto uliopo eneo la Nguzonane mjini Shinyanga ambapo Mhe. Zitto Kabwe amesema mpaka ifikapo mwishoni mwa Mwaka huu Tanzania iwe na sheria ya mabadiliko ya katiba na kwamba mswaada wa sheria uwe umepelekwa bungeni mapema.

Pamoja na mambo mengine kiongozi huyo wa ACT Wazalendo ameitaka serikali kuongeza uwezo wa wakala hifadhi ya chakula Nchini, NFRA kununua chakula cha kutosha na kukitunza  hali itakayowawezesha wananchi kununua kwa gharama nafuu.

“Ili tuwe na katiba mpya ni lazima turekebishe sheria ya mabadiliko ya katiba na ndiyo maana ACT Wazalendo tunapambana tunapigania kwamba mpaka itakapofika mwishoni mwa Mwaka huu tuwe na sheria ya mabadiliko ya katiba mpya mswaada wa sheria ya mabadiliko ya katiba upelekwe bungeni ili kurekebisha sheria ya mabadiliko ya katiba ya Mwaka 2011 tuweze kutengeneza mtililiko mpya wa namna gani ambavyo tunakwenda kukamilisha chakato wa katiba”.amesema Mhe. Zitto

“Serikali iongeze uwezo wa NFRA kununua chakula cha kutosha na kukitunza ili wakati wa bei kubwa sana waweze kuingiza sokoni watu mpate chakula cha bei nafuu nah ii inawezekana kwa sababu chakula ni mahitaji ya msingi ya kila mtu kwahiyo ACT Wazalendo tunapambana kwa ajili ya gharama nafuu za maisha na tumeeleza katika mpango wetu huu wa Taifa la wote maslahi ya wote lazima uwe na gharama nafuu za maisha mahitaji ya msingi ya mwananchi yawe nafuu ili aweze kufanya shughuli za uzalishaji na uchumi wa Taifa uweze kukua”.amesema Mhe. Zitto

Aidha kiongozi huyo amezungumzia mambo mbalimbali yanayogusa sekta ya Elimu, Afya pamoja na miundombinu huku akiwaomba wananchi wa Mkoa wa Shinyanga kujiunga na chama hicho na kushirikiana ili kuleta mabadiliko chanya kwenye jamii na Taifa kwa ujumla.

Awali akizungumza katika mkutano huo Bahati Chirwa ambaye ni Naibu Waziri kivuri Elimu amezungumzia kuhusu fursa kutolewa kwa misingi ya upendeleo.

“Kuna kata hapa hazijafikiwa na umeme ikiwemo kata ya Mwawaza na Chibe lakini kuna vijana mnahitaji ajira na vijana wengi mlitakiwa mpatiwe mikopo inayotolewa na Halmahauri ili muweze kujiajiri lakini mikopo haitolewi na ikitolewa inatolewa kwa upendeleo, vikundi vya madiwani na wengine ambao hawahusiki na hiyo mikopo”.amesema Naibu waziri Kivuri Elimu

Kwa upande wake makamu mwenyekiti wa chama cha ACT Wazalendo  Tanzania bara Bi. Dorothy Semu amezungumzia  kuhusu maboresho ya kikokotoo kwa wastaafu ambapo amesema muhimu serikali kutoa mafao bora kwa wastaaru.

Naye mjumbe wa Halmashauri kuu ya ACT Wazalendo Taifa Bwana Msafiri Mtemelwa amewaomba wananchi kuendelea kukiamini chama hicho katika kuleta maendeleo.

Chama cha ACT Wazalendo kimeendelea na ziara ya kutembelea mikoa mbalimbali Nchini kwa kufanya mikutano ya hadhara ikiwa ni mwendelezo pia wa kampeni ya chama hicho  inayoitwa brand promise ambayo ilizinduliwa rasmi Mwezi March Mwaka huu jijini Dar es salaam.

Kiongozi wa Chama cha ACT Wazalendo Taifa Mhe. Zitto Kabwe akizungumza na wananchi leo Juni 6,2023 katika mkutano wa hadhara mjini Shinyanga.

Makamu mwenyekiti wa chama cha ACT Wazalendo  Tanzania Bara Bi. Dorothy Semu akizungumza kwenye mkutano wa hadhara leo Juni 6,2023 katika uwanja wa zima moto mjini Shinyanga.

Bahati Chirwa ambaye ni Naibu Waziri kivuri Elimu akizungumza kwenye mkutano wa hadhara leo Juni 6,2023 katika uwanja wa zima moto mjini Shinyanga.

Mjumbe wa Halmashauri kuu ya ACT Wazalendo Taifa Bwana Msafiri Mtemelwa akizungumza kwenye mkutano wa hadhara leo Juni 6,2023 katika uwanja wa zima moto mjini Shinyanga.


Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



BBC NEWS