Header Ads Widget

DIWANI WA KATA YA NDEMBEZI MHE. VICTOR MMANYWA AFANYA MKUTANO WA HADHARA KUSIKILIZA KERO MTAA WA BUTENGWA

Na Mapuli Misalaba, Shinyanga.

Diwani wa kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga Mhe. Victor Thobias Mmanywa leo ameanza ziara kutembelea mitaa yote kwenye kata hiyo kwa lengo la kusikiliza kero na changamoto  mbalimbali zinazowakabili wananchi ili kuzitafutia ufumbuzi.

Diwani huyo ametembelea mtaa wa Butengwa ambapo baadhi ya wakazi wa mtaa huo wamempongeza kwa utendaji wake ambapo wametaja kero na changamoto mbalimbali zinazowakabili ikiwemo changamoto ya miundombinu ya barabara, maji, umeme pamoja na afya.

Wamesema mpaka sasa hakuna barabara za mitaa zilizochongwa, wameomba kujengewa kituo cha afya karibu ili kuepusha changamoto ya mama wajawazito kujifungulia nyumbani, wameomba kujengewa soko pamoja na stendi katika eneo hilo huku baadhi yao wakilikata jina la Butengwa na wengine kupendekeza jila la Mji mwema au Majiclub.

Wamesema jina la Butengwa linachangia baadhi ya shughuli za kijamii kutofanikiwa pamoja na shughuli zingine zinazotokana na serikali kwa Imani ya kuwa wametengwa na jamii inayowazunguka.

Wamemuomba Mh. Diwani kushughulikia changamoto zinazowakabili ambapo  baadhi yao wametaja changamoto za ardhi huku wakiomba wataalam kwenda kupima maeneo yao ili wapate hati miliki.

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Ndembezi Mhe. Victor Thobias Mmanywa ameahidi kutatua changamoto zilizopo kadri ya uwezo wake huku zingine akitaja kuzifikisha sehemu husika ili ziweze kushughulikiwa kwa wakati.

Amewaomba wakazi wa mtaa wa Butengwa kuendelea kumwamini na kushirikiana naye katika kuleta maendeleo ambapo amesema atahakikisha changamoto zinapungua katika sekta mbalimbali ikiwemo changamoto ya barabara, maji, afya, umeme pamoja na elimu.

Amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, Mbunge wa jimbo la Shinyanga mjini Mhe. Paschal Patrobas Katambi pamoja na viongozi wengine wa serikali katika Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kwa kutenga na kupitisha fedha katika miradi iliyokamilika pamoja na miradi inayoendelea ikiwemo ujenzi wa shule ya wasichana Butengwa kata ya Ndembezi.

“Mimi nimethamiria tena kwa thamira ya dhati kabisa kuwatumikia wananchi wa Ndembezi katika nafasi hii na Butengwa nawaahidi sitoaangusha nitahakikisha kero zinaenda kuisha kabla sijamaliza muda wangu Mwaka 2025, nitahakikisha changamoto kama siyo kuisha basi tunafikia asilimia 95 lakini babari ya maji, umeme na barabara ninaamini tutafikia asilimia 98 au kumaliza kabisa”. amesema Mhe, Mmanywa

“Changamoto ya kituo cha afya tuna jengo letu wana Butengwa naomba niwahakikishie kituo hiki tutakiendeleza kwa ajili ya kupata huduma za afya wananchi wetu wa huku wote na bajeti ya kuanzia Mwezi wa saba mtaona, tayari kuna Milioni mia mbili zimeshatengwa kwa ajili ya kumalizia hili jengo”

“Mmeomba Butengwa kuwa jina hili linakasolo ndiyo maana mmetengwa nimelichukua nitalifikisha kwenye vikao vya maamuzi, lakini pia tayari nimeomba tupewe eneo lingine kwa ajili ya soko na changamoto ya eneo la malalo nitaendelea kuwa bega kwa began a ninyi ili kuhakikisha hapa Butengwa mnapata eneo la malalo kwa wenzetu wanaotangulia mbele za haki”amesema Mhe, Mmanywa

Diwani wa kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga Mhe. Victor Thobias Mmanywa ameanza ziara Jumatatu Juni 5,2023 kutembelea mitaa yote ya kata hiyo ikiwa lengo ni kupokea na kutatua changamoto zinazowakabili wananchi ambapo leo ametembelea mtaa wa Butengwa na kwamba ziara hii ni endelevu.

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



BBC NEWS