Header Ads Widget

MWANAFUNZI ALIYEZAMA KWENYE MAJI KWA SIKU SABA NJOMBE AZIKWA LEO

 


Na Gabriel Kilamlya Matukio DaimaAPP NJOMBE


Mamia kwa maelfu ya wakazi wa Njombe wamejitokeza katika Mazishi ya Anaida Deusi Mgaya (12) aliyekuwa mwanafunzi wa darasa la nne katika shule ya msingi Mdete aliyefariki   kwa kuzama kwenye maji akitoka shuleni baada ya mvua kubwa kunyesha na kutafutwa katika kipindi cha siku saba.


Katika mazishi hayo yaliyoongozwa kwa ibada na mchungaji wa kanisa la EAGT Ibrahim Mtonyole,historia ya  Mtoto huyo imesomwa na Babu wa marehemu mzee Jocob Lilawola ikisema mtoto huyo  alizama katika mto Makinda na kupatikana siku ya saba katika mto Ruhuji.


Afisa elimu mkoa wa Njombe Nelasi Mulungu kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Njombe ametoa salaam za rambirambi akitaka mshikamano wa pamoja katika kipindi hiki kigumu kwa familia na shule ya  msingi mdete.




Baadhi ya viongozi wa chama na serikali akiwemo Erasto Mpete mwenyekiti wa Halmashauri ya mji wa Njombe Alatanga Nyagawa Diwani wa Kata ya Njombe Mjini na Samuel Mgaya mwenyekiti wa UVCCM Mkoa kwa niaba ya Chama cha mapinduzi wamesema kila mmoja anao wajibu wa kulinda watoto badala ya kuwaacha peke yao hata wanapokutwa katika mazingira magumu na hatarishi.


Kwa upande wake Kamanda wa Polisi mkoa wa Njombe Hamis Issa amesema hakuna sababu ya kulaumiana katika suala hilo kwani limeshatokea na hivyo kinachotakiwa ni umakini katika kuwalinda watoto.


Daitan Lutumo Janeth Mtewele na Mashaka Kawogo Ni wakazi wa Njombe walioshiriki kutafuta mwili huo katika siku zote tangu Tarehe 14 Februari ambao wameeleza masikitiko juu ya msiba huo uliogusa hisia za watu wengi.


Mtoto Anaida Mgaya amemaliza safari yake ya duniani na kupumzishwa katika makaburi ya Kilimani Mjini Njombe.


Bwana Alitoa na bwana Ametwaa jina lake lihimidiwe.



Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI