Header Ads Widget

JESHI LA POLISI LAWAJIBU ASKARI WANAOLALAMIKA.

 


Wakati askari wakilalamika kupunjwa mishahara na posho wanazostahili, Jeshi la Polisi limeishukuru Serikali kwa jinsi inavyolijali kwa kuhakikisha posho na stahiki nyingine zinalipwa kwa wakati.

 

Taarifa iliyotolewa na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP), David Misime ambaye ni msemaji wa jeshi hilo kutoka makao makuu jijini Dodoma, imesema licha ya stahiki za askari wake, Serikali inalipa fedha za mafuta na vipuri vya magari yanayopelekwa hadi kwa wakuu wa polisi wa wilaya ili kufanikisha utendaji wao.

 

“Jeshi la Polisi linaishukuru Serikali ya awamu ya sita kwa namna inavyolijali kwa mambo mbalimbali, kwani ni kipindi ambacho kwa kiasi kikubwa tumeshuhudia posho na stahiki mbalimbali za askari zikiendelea kulipwa kwa kasi kubwa kuhakikisha kila askari anapata posho anayostahili,” alisema

 

 

Ingawa askari wenyewe wanasema utaratibu umebadilika tangu Serikali izuie kukatwa fedha zao za posho ya chakula kila wanapoenda kwenye mafunzo, Misime amesema Serikali imetoa Sh11 bilioni kuwagharimia mafunzo yao na Sh11.7 bilioni kwa ajili ya sare za askari wote wa jeshi hilo wanaozidi 40,000.

 

“Hayo yote yamefanywa na Serikali ili kuboresha maslahi na vitendea kazi kwa askari polisi. Zipo taratibu za askari kuwasilisha madai yake halali zinazofahamika kwa wote,” alitahadharisha Misime.

 

Katika jitihada za kuhakikisha askari wanafika eneo la tukio kwa wakati, wanadhibiti uhalifu uliopangwa na kuwalinda raia na mali zao kwa uhakika, Misime amesema Serikali imetoa Sh15 bilioni kwa ajili ya kununua magari na tayari 80 yameshapokelewa na kusambazwa mikoani.

 

Magari mengine 72 amesema yanakamilisha utaratibu wa usajili ili yasambazwe mikoani na vikosini, huku magari mengine pamoja na pikipiki 336 kwa ajili ya doria yakiwa yameagizwa.

 

Kwa magari hayo na uwezeshaji mwingine uliofanywa na Serikali kwa Jeshi la Polisi, Misime amesisitiza kwamba “askari anayekwenda kwa raia na kudai ampe fedha ya mafuta ya gari, akibainika, hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake."

Post a Comment

0 Comments



MAGAZETI



NAMBA ZA HUDUMA YA USAFIRI WA KUKODI