NA TITUS MWOMBEKI, Matukio Daima App Kagera.
Mradi wa kuzalisha umeme katika maporomoko ya Rusumo uliopo wilayani Ngara mkoani Kagera unatarajiwa kukamilika Novemba mwaka huu.
Mradi huo utakaozinufaisha nchi za Tanzania, Rwanda na Burundi tayari umekamilika kwa asilimia 95.
Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dk Emmanuel Tutuba katika ziara maalumu ya kukagua mradi huo.
Dk Tutuba ambaye aliambatana na wasimamizi wakuu wa mradi huo alisema mradi huo utazalisha megawati 80 za umeme na kila nchi itanufaika kwa kupata megawati 27.
“Tumetembelea kituo cha kuzalisha umeme, tumeona ujenzi wake umeisha kamilika kwa kiwango kikubwa na wahandisi wametuahidi kuwa ifikapo mwezi Novemba mwaka huu watatukabidhi mradi wetu, kwa sababu ni makubaliano baina ya nchi tatu kwamba megawati 80 zitakazozalishwa, kila nchi itakuwa na fursa ya kutumia theluthi moja”alisema Dk Tutuba.
Aidha Katibu mkuu huyo wa Wizara ya Fefha aliilekeza halmashauri ya Ngara mkoani humo kuweka mpango endelevu wa kutunza vyanzo vya maji, ili yale maji yaendelee kutililika kwenye mto na kuusaidia kuleta maji katika mitambo ya kuzalisha umeme.
Katika hatua hiyo, Dk Tutuba pia aliisisitiza halmashauri hiyo kushughulikia fidia za wananchi wanaomiliki maeneo ya mradi huo kwa haraka ili waweze kuondoka.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wizara ya Nishati, Felchesmi Mramba alisema kuwa mradi huo utasaidia uzalishaji wa umeme mwingi si kwa matumizi ya mkoa wa Kagera tu bali na mikoa ya jirani ukiwemo Mkoa wa Kigoma.
“Mnafahamu kuwa mkoa wa Kagera umekuwa ukitumia umeme kutoka nchi ya Uganda hivyo basi, mradi huu ukikamilika utasaidia kuunganishwa na miradi mingine ya umeme ukiwemo wa kutoka Benaco keelekea Kyaka kupitia Nyakanazi ili kusaidia Mkoa wa Kagera kuanza kupata umeme kutoka kwenye gridi ya Taifa”
Mradi wa kuzalisha umeme katika maporomoko ya Rusumo ulianza utekelezaji wake mwaka 2017 kwa kuzihusisha nchi za Tanzania, Rwanda na Burundi kwa udhamini wa Benki ya dunia (WB) iliyotoa mkopo nafuu wenye thamani ya Dola za Marekani milioni 340, pamoja na Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB) iliyotoa Sh milioni 120 ukitarajiwa kukamilika mwaka 2020.
Mradi huo unajengwa na Kampuni za CGCOC Group and Jiangxi Water ang Hydropower Construction Company (JWHC) China, kutoka nchini China, India na Ujerumani.
0 Comments