Na Chausiku Said Mwanza.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Mhandisi Robert Gabriel amekemea vitendo vya wizi wa vifaa vya ujenzi wa daraja la JPM linalojengwa hali inayosababisha ujenzi huo kutokamilika kwa wakati.
Kauli hiyo ameitoa leo julai 4, 2022 wakati akiwa ameambatana na kamati ya Mkoa na Wilaya katika ziara ya ukaguzi wa daraja hilo linalounganisha wananchi wa kigongo feli na Bisisi na kujionea namna ujenzi unavyoendelea katika daraja hilo.
Mhandisi Gabriel amefafanua kuwa mtu yeyote atakayekamatwa na kifaa chochote chenye asili ya mradi wa ujenzi wa daraja atachukuliwa hatua za kisheria.
"Niendelee kulipongeza jeshi la Polisi na kuanzia leo tutaongeza ulinzi kwenye daraja hili, ili kuhakikisha vyuma na vifaa vinavyotumika vinabaki kuwa salama na kuanzia eneo la mita 300 kulia na kushoto mwa daraja hili litakua kwenye ulinzi pamoja usalama wa wavuvi" Alisema Mhandisi Gabriel.
Aidha amewataka wafanyakazi wanaofanya kazi katika daraja hilo kulidhika na mishahara yao wanayoipata na kuhakikisha wanakuwa wazalendo katika kutekeleza majukumu yao pamoja na kutunza vifaa wanavyotumia katika ujenzi wa daraja hilo.
"Uzalendo hapa uwe ndio dira yetu, viongozi na wananchi tuwe wasimamizi wa pamoja kwenye mradi huu ili kuhakikisha vifaa na mitambo vinatunzwa na mradi unakamilika ndani ya muda uliokusudiwa." Alisema Mhe Gabriel.
Hata hivyo amemtaka Mkandarasi CCECC kuongeza spidi ya Ujenzi wa Daraja la JPM lenye urefu wa KM 3.2 na na kuhakikisha wanakuwa wazalendo katika kutunza vifaa vya ujenzi.
Kwa upande wake Mkandarasi Mshauri wa Mradi Abdulkarim Majuto amesema kuwa ujenzi wa daraja la JPM umefikia asilimia 47.4 na nguzo 21 kati ya 67 tayari zimewekwa ndani ya mwezi Julai pamoja na kuweka nguzo ulalo na zege ya juu.










0 Comments