Na Gift Mongi,Matukio DaimaAPP,Moshi
Kufuatia jitihada za serikali kutoa fedha kiasi cha milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Moshi baadhi ya wananchi wa jimbo hilo wameonyesha kukubali jitihada hizo ambapo wamesema kwa kipindi kirefu ilishindikana na kuwa sasa itaenda kubaki historia
Wananchi hao wametoa kauli hiyo ikiwa ni siku chache mara baada ya mbunge wa jimbo la Moshi Vijijini Prof Patrick Ndakidemi kuishukuru serikali kwa hatua hiyo ambapo itaenda kuondoa adha kwa wakazi wa jimbo hilo
Mkazi wa Kibosho Kirima Emmanuel Ollomi alisema kujengwa kwa hospitali hiyo ni mafanikio makubwa kwa wakazi wa jimbo la Moshi Vijijini na kuwa hayo ni matokeo ya kuwa na uwakilishi sahihi ambao unajali hali za wananchi wake.
"Tuna mbunge sahihi na ndio maana ameweza kwenda kuishawishi serikali na sasa tunaenda kupata Hospitali yetu ya wilaya jambo ambalo lilishindikana kwa kipindi kirefu hakika huu ndio uwakilishi tuliokuwa tunautaka siku nyingi"alisema
Baraka Mushi mkazi wa Kindi Kibosho alisema wananchi wa jimbo hilo kwa kipindi kirefu walikosa Hosipitali ya wilaya jambo lililowaongezea gharama wakati wa kwenda kutafuta matibabu katika hospitali nyinginezo ikiwemo ile ya rufaa ya Mawenzi.
Agripina Mmasy mkazi wa Uru Shimbwe alisema serikali kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa awamu ya kwanza ni dhamira njema katika keleta maendeleo kwa wananchi wa jimbo hilo na hivyo mbunge wao Prof Patrick Ndakidemi hana budi kuendelea kufuatilia kiwango kilichobaki ili iweze kukamilika kwa wakati.
Akichangia bungeni wiki hii mbunge wa Moshi Vijijini Prof Patrick Ndakidemi alisema baada ya kipindi kirefu wilaya hiyo kukosa Hospitali ya wilaya sasa serikali kilio hicho kimeenda kufikia tamati baada ya serikali kutoa fedha kiasi cha milioni 500 na ujenzi umeanza katika kata ya Mabogini.
"Mbali na kutolewa kwa fedha hizo tayari jitihada za kuanza kwa mchakato wa ujenzi wa hospitali hiyo umeshaanza mara moja lengo hapa ni kuhakikisha malengo ya serikali yanaenda kutimia"alisema Prof Ndakidemi
Hata hivyo katika hatua nyingine Prof Ndakidemi aliishukuru Halmashauri ya Moshi kwa kupata hati safi kwa miaka sita mfululizo na hivyo kutumia muda huo kuwapongeza mkurugenzi na mkuu wa wilaya pamoja na watumishi wa halmashauri katika matumizi sahihi ya fedha za umma.
Mwisho
0 Comments