Teddy Kilanga _ARUSHA
Maonesho ya kimataifa ya kilimo yanayojulikana Kama "TANZFOOD Expo "yanayofanyika jijini Arusha katika viwanja vya magereza vilivyopo mkoani Arusha kuanzia yameanza rasmi leo machi 11,2022 kwa lengo la kukuza mnyororo wa thamani katika sekta hiyo.
Zaidi ya makampuni 120 kutoka Tanzania na nchi jirani za Afrika Mashariki yameshiriki katika maonesho hayo ambayo yameandaliwa na kampuni ya KILIFAIR Promotion kwa lengo la kuhamasisha na kukuza sekta ya kilimo.
Akizindua maonesho hayo jijini Arusha,Mkuu wa mkoa wa Arusha,John Mongella alisema maonesho hayo yataleta tija katika mnyororo mzima wa thamani katika kilimo ,ufugaji,uvuvi pamoja na uchakataji.
"Kwa hiyo hapa utaonekana utaalamu wa mazao,teknolojia za kilimo,za ufugaji pamoja na za uchakataji ambapo wadau wa kilimo watapata fursa za elimu katika kujifunza na biashara,"alisema Mongella.
Pia alisema fursa nyingine ni katika kilimo,ufugaji ,uvuvi pamoja na mengine yahusiyo sekta hiyo ikiwemo masoko na biashara hivyo wanawashukuru KILLIFAIR kwa kuandaa maonesho hayo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wakiwemo TAHA.
"Maonesho hayo kama serikali ya mkoa wa Arusha tumepania kuyafanya kimataifa na ajenda yetu ni kuufanya mji huu wa Arusha kuwa wa matukio,"alisema.
Mmoja wa wakurugenzi wa KILIFAIR Promotion ,Dominic Shoo aliwaomba wananchi mbalimbali kutembelea maonesho hayo kwa ajili ya kujifunza pamoja na kufanya biashara pia kukutana na wadau wa kilimo katika kubadilishana mawazo ikiwemo kubadilishana changamoto na fursa.
"Tumeona kuna nafasi kwa upande wa kilimo kwa baadhi ya watu kushindwa kuwafikia wadau wa kilimo kwa wakati kwani lengo letu la maonesho haya ni kuwakutanisha wanunuzi pamoja na wazalishaji wa mazao,"alisema Shoo.
Shoo alisema kutokana na Ombwe la elimu pia wameona kupitia maonesho hayo watatoa mafunzo mbalimbali kutoka kwa wataalamu wa kilimo hapa nchini Tanzania kwa lengo la kumjenga mkulima katika kutengeneza faida ya mazao anayozalisha.
Kwa upande wake Naibu Katibu mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki(EAC) Christoph Bazivamo aliipongeza Kilifair kwa kuandaa maonesho hayo ambayo yatakuza mnyororo wa thamani katika sekta ya kilimo kutokana na uzalisha uliopo kwenye viwanda katika jumuiya ya Afrika ya mashariki.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa TAHA,Dk.Jackline Mkindi ambaye pia ni mwenyekiti wa baraza la kilimo Tanzania alisema sekta ya kilimo imefunguka katika sekta hiyo ambayo ndio inashikilia uchumi wa Taifa na masoko yamefunguka sana ikiwa bidhaa za nchini hapa zinagombaniwa kwenye masoko ya kimataifa.
"Lakini tunavyoogelea masoko ya kimataifa ni vyema kutokusahau kuwa Tanzania kuwa imezungukwa na nchi nyingi barani Afrika ambazo zinahitaji bidhaa kutoka Tanzania hivyo maonyesho kama haya yanatupa fursa vilivile ni chachu kwa watanzania kupitia sekta binafsi,"alisema Dk.Mkindi.
Aidha alisema kupitia maonyesho hayo yameleta wasindikaji kutoka nchi ya Kenya,Rwanda,Burundi pamoja na nchi nyingine kwa hiyo kujifunza ni jambo la muhimu katika kuendelea kuongeza tija kwenye uzalishaji lengo kubwa ni kubadilishana mawazo na Taarifa.
Dk.Mkindi alisema bila kuwa na taarifa muhimu wazalishaji hawezi kufikia masoko ikiwa wao kama TAHA waliweza kushiriki katika mikutano mikubwa ya kimataifa ambapo walikuwa Dubai,Ufaransa pamoja na Ubelgiji ikiwa lengo kubwa ni kuangalia fursa za masoko.
"Naomba ni wahakikishie kwamba fursa katika sekta ya kilimo ni kubwa haso katika mazao ya mboga na matunda kwani Dunia inahitaji matunda ,mboga na viungo kutoka nchi ya Tanzania kwa hiyo napenda ni hamasishe watanzania wenzangu tuwekeze kwenye kilimo na kwa akili huku tukitafuta taarifa muhimu,"alisema Dk.Mkindi.
Alisema pamoja na kupata taarifa muhimu pia wataona namna gani ya kuweza kujengeana uwezo ili waweze kushindana kimataifa hivyo anapenda awahakikishie kuwa masoko yapo.
0 Comments