BODI ya nafaka na mazao mchanganyiko (CPB) kanda ya nyanda za juu kusini imesema kuwa pamoja na zoezi linaloendelea na uuzaji wa mahindi nje ya nchi ila bado hifadhi ya mahindi katika vituo vyake ni kubwa zaidi na bei ya mahindi haijapanda sana ukilinganisha na mwaka 2016.
Kuwa mwaka 2016 bei ya mahindi mwezi kama huu Januari ilifikia hadi shilingi 1050 ila kwa mwaka huu bei ya mahindi kwa kilo ni kati ya shilingi 500 hadi 600 kwa kilo moja hivyo hali ya chakula bado ni nzuri na haitegemewi kuwa mbaya maana akiba ya mahindi waliyonayo ni kubwa .
Akizungumza Leo na Matukio Daima Media kwa niaba ya meneja wa Bodi ya nafaka na mazao mchanganyiko kanda ya nyanda za juu kusini Anganyila Kamihanda alisema kuwa lengo kubwa la taasisi hiyo ni kuendelea kufanya biashara na sasa biashara kubwa ni uuzaji wa zao la mahindi ambalo siku za nyuma hali ya uuzaji wa mahindi ilikuwa mbaya zaidi kabla ya serikali kuruhusu mazao kuuzwa nje ya nchi .
“ Ikumbukwe hapa kati kati hali ya uuzaji wa mahindi ilikuwa mbaya hadi kupelekea hifadhi zetu kujaa ila sasa tumefanikiwa kupunguza akiba kubwa ya mahindi tuliyokuwa nayo kwa kupitia mikataba ya ununuzi wa mahindi tuliyoingia na kampuni za Rwanda na Kenya “ alisema
Alisema katika kituo cha Iringa walikuwa na hifadhi ya mahindi ambapo walikuwa na tani 18,000 za mahindi kabla ya Rwanda kununua tani 5000 hivyo akiba ambayo watabaki nayo ni tani 13000 za mahindi ambayo wanaendelea kusaga unga na kusambaza ndani ya nchi kwa gharama nafuu zaidi .
Pia alisema kwenye vituo vingine vya Songwe na Songea mkoa wa Ruvuma bado wanayo hifadhi ya kutosha ya mahindi na kama hali ya ukame itaendelea bado hakutakuwa na hofu yoyote maana hifadhi ya mahindi iliyopo ni kubwa zaidi kwao na pia hifadhi ya Taifa ya chakula wana akiba ya kutosha ya mahindi .
Alisema kuwa ikitokea mahindi yamepungua watakwenda kuchukua mahindi kwenye hifadhi ya Taifa ya nafaka ambako kuna akiba ya kutosha ya mahindi .
Alisema kuwa kwa kawaida bei ya mahindi iliyopo ni nzuri sana na nafuu kwa wananchi kwani kama bei ya mahindi ingepanda mwezi wa 9 ama wa 10 ndipo huwa mbaya zaidi ingefikia bei hiyo kwa miezi tajwa basi hofu ingekuwa kubwa zaidi lakini pamoja na changamoto za mvua zilizokuwepo bei ya mahindi haitapanda badala yake mwakani wakulima watakuwa na neema zaidi ya bei nzuri ya mazao .





0 Comments